SERIKALI kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini imetenga bajeti ya maendeleo ya mwaka wa fedha 2021/2022 ya kiasi cha Sh bilioni mbili kununua magari mapya ya kisasa ya kuzima moto. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 16 Februari, 2022 bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Jumanne Sagini wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti maalumu, Ether Matiko.
Matiko ameuliza je, ni lini Serikali itanunua magari ya kisasa ya zimamoto ili kunusuru maisha ya raia na mali zao.
Akijibu swali hilo, Sagini amesema serikali imeandaa mpango mkakati wa kuimarisha huduma ya zimamoto na uokoaji nchini kwa kuimarisha na kuongeza vifaa vya kisasa vya utendaji kazi katika Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.
Amesema vifaa hivyo vya kisasa vitaenda sambamba na upelekaji wa huduma ya zimamoto na uokoaji katika Wilaya zote ambazo hazina huduma hiyo.
Amesema Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini imetenga bajeti ya maendeleo ya 2021/2022 ya kiasi cha Shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kununua magari mapya ya kisasa ya kuzima moto.
“Lengo kuu la ununuzi wa magari haya ni kuongeza ufanisi kwenye shughuli za kuokoa maisha na mali za wananchi, pindi patokeapo ajali za moto na nyingine.
“Taratibu zote za ununuzi zikikamilika, magari ya kuzima moto yatapelekwa katika Mikoa isiyokuwa na huduma ya Zimamoto na Uokoaji. Serikali itaendelea kutenga fedha kila mwaka ili kuliwezesha vitendea kazi stahiki Jeshi la Zimamoto na Uokoaji,” amesema.
Leave a comment