MBUNGE wa Kibamba (CCM), Issa Mtemvu, ameitaka Serikali ifanye ukaguzi maalumu wa asilimia 10 ya fedha za mapato ya halmashauri nchini, zinazotolewa kwa ajili ya mkopo kwa wananchi wa makundi maalumu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mtemvu ametoa wito huo leo Jumatano, tarehe 16 Februari 2022, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
Mbunge huyo Kibamba, jijini Dar es Salaam, amedai kuna wilaya moja katika jiji hilo ina ubadhirifu mkubwa wa fedha hizo.
“Yapo malalamiko mengi sana ya fedha hizi, takribani Sh. 60 bilioni ambazo zinarudi kila mwaka kutokea kwenye fungu hili la asilimia 10. Imeonesha Dar es Salaam kwenye wilaya moja wapo, tayari kuna ubadhirifu mkubwa sana wa fedha hizi,” amesema Mtemvu na kuongeza:
“Serikali haioni ni wakati sasa wa kupeleka ukaguzi maalumu kwa nchi nzima, ili tupate tathimini ya kweli?”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Dk. Festo Dugange, amesema Serikali italianyia kazi ombi hilo.
“Kama kutakuwa na sababu ya kutazama uwezekano wa kufanya ukaguzi maalumu, tutalifanya sababu kazi ya Serikali ni kudhibiti fedha hizo, ili ziweze kuleta tija kwa watarajiwa. Tumechukua wazo la mbunge na tutalifanyia kazi,” amesema Dk. Dugange.
Aidha, Dk. Dugange amesema wizara yake inafanya tathimini ya kuona halmashauri zilizofanikiwa na zisizofanikiwa katika utoaji na urejeshaji mikopo hiyo, ili kuwa na udhibiti mzuri wa fedha hizo.
“Kweli kumekuwa na malalamiko ya baadhi ya maeneo nchini kote, kuhusiana na matumizi ya fedha za asilimia 10 na Serikali tunafanya tathimini ya kuona wapi kuna mafanikio, maeneo gani yana changamoto na changamoto ni zipi,” amesema Dk. Dugange na kuongeza:
“ Ili sasa baada ya tathimini hiyo tuwe na direction, ambayo itatuwezesha kuwa na fedha itakayoleta tija kwa wananchi wetu.”
Fedha hizo hutolewa na halmashauri zote nchini, kwa ajili ya mikopo ya makundi maalum, ambayo ni kina mama, vijana, wazee na watu wenye ulemavu.
Leave a comment