RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Serikali tayari imetumia jumla ya Sh bilioni 596.3 kwa ajili ya ununuzi wa ndege nyingine tano mbali na tatu ambazo zimenunuliwa na kuletwa nchini hivi karibuni. Anaripoti Mwandishi wetu (endelea)
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Oktoba, 2021 jijini Dodoma wakati akizindua mpango wa kampeni ya maendeleo kwa ustawi na mapambano ya UVIKO -19 ambao umetokana na mkopo nafuu wa Sh trilioni 1.3 uliotolewa na Shirika hilo la IMF.
Aidha, akielezea tathmini ya kipindi cha miezi sita ambayo amekaa madarakani kuanzia tarehe 19 Machi mwaka huu, Rais Samia amesema kuhusu sekta ya anga imeendelea kuimarika kwani hivi karibuni Serikali imesaini mkataba wa ujenzi wa uwanja wa ndege wa msalato hapa Dodoma.
Amesema upanuzi wa viwanja vingine, ikiwamo Mtwara, Songea na Iringa unaendelea.
“Ndege tatu zilizonunuliwa na serikali zote zimewasili hivyo kufikisha idadi ya ndege 11.
“Serikali imesaini mkataba wa ndege tano mkataba wa ununuzi wa ndege nyingine tano aina ya Dreamliner 1, Boeing 2, Ndege ya mizigo moja na Bomberdier Dash Q4100,” amesema.
Aidha, amesema kuhusu usafiri wa barabara, nyingi zinaendelea kujengwa sehemu mbalimbali nchini.
Akitolea mfano mkoani Dodoma amesema tayari kumeanza ujenzi wa barabara ya mzunguko ya njia nne.
“Hata ile barabara ya njia nane Dar es Salaam ambayo iliripotiwa kusimama, nataka kuwahakikishia inaendelea na iko kwenye za mwisho za mabadiliko.
“Lakini tunakwenda na kuanza ujenzi wa njia nne nne hapa Dodoma, upande wa kwenda Singida, Dar es Salaam na Arusha,” amesema.
Leave a comment