MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umefanya ziara katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, kwa ajili ya kuboresha mikakati ya utoaji huduma za utetezi wa haki za binadamu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo Jumatano, tarehe 11 Agosti 2021, jijini Mwanza, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema dhumuni la ziara hiyo ni kuangalia maeneo ya kanda hiyo, ambayo hayafikiwi na huduma za utetezi wa haki za wanadamu.
“Ziara hii inalenga kujua maneneo ambayo hayana wadau wa kutosha, kujua maeneo ya kuboresha huduma za mtandao kwa wanachama,” amesema Olengurumwa.
Aidha, Olengurumwa amesema ziara hiyo imelenga kufuatilia utendaji wa wanachama 30 wa THRDC, walioko katika mikoa ya kanda hiyo, Mwanza, Simiyu na Mara.
“Dhumuni kuu la ziara hii kwa wanachama wa mtandao, ni kuweza kuona kazi mbali mbali zinazofanywa na wanachama wa mtandao, maendeleo, mafanikio na changamoto za kiusalama, wanazopitia katika kutetea haki za binadamu katika kanda zao,” amesema OIlengurumwa.
Olengurumwa amesema, THRDC itaendelea kuimarisha huduma zinazotolewa na mtandao huo, ikiwemo utetezi wa haki ya uhuru wa kujieleza, haki za wafugaji, haki za wanawake, haki za watoto, utoaji wa huduma na msaada wa kisheria na utetezi wa haki za kijamii na uwajibikaji.
Huduma nyingine ni, utetezi wa rasilimali, maliasili na haki za kiuchumi, uhuru wa kujieleza na haki za makundi maalum.
Leave a comment