MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umeviomba vyombo vya dola kuzipa kipaumbele kesi za ukatili wa kijinsia, zinazoripotiwa na watetezi wa haki za binadamu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatano, tarehe 11 Agosti 2021, jijini Mwanza na Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, katika ziara yake ya kikazi kwenye Kanda ya Ziwa, iliyoanza tarehe 9 Agosti mwaka huu.
Mratibu huyo wa THRDC amesema, kesi hizo zikipewa kipaumbele, itasaidia kupunguza uvunjwaji wa haki za binadamu nchini.
“Tunatoa wito kwa vyombo vya dola, kuzipa kipaumbele kesi zaa ukatili wa kijinsia zinazoripotiwa na watetezi wa haki za binadamu. Hii itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa kasi ya wimbi la uvunjwaji wa haki za binadamu,” amesema Olengurumwa.
Aidha, Olengurumwa amewaomba watetezi wa haki za binadamu, kushirikiana na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), kutokomeza ukatili huo.
“Natoa wito watetezi wa haki za bindamu kuungana na mashirika mengine yanayotetea haki za binadamu kuwa na sauti ya pamoja,” amesema Olengurumwa.
Olengurumwa ameongeza “kwa mfano mashirika yanayojihusisha na masuala ya ukatili wa kijinsia na utetezi wa haki za watoto, kuwa na sauti ya pamoja ili kuweza kufikisha agenda zao muhimu kupitia majukwaa ya kitaifa na kimataifa yanayohusu haki za binadamu.”
Akizungumzia ziara yake katika kanda hiyo, Olengurumwa amesema THRDC imetembelea wanachama wake 30 walioko kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa, kwa ajili ya kuangalia utekelezaji wake.
Leave a comment