KATIBU Mkuu mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo, amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, aboreshe maslahi ya watumishi wa umma, kama Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho 2020-2025, inavyoelekeza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Chongolo ametoa wito huo leo Jumamosi tarehe 1 Mei 2021, katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazo duniani ‘Mei Mosi’, iliyofanyika jijini Mwanza, ambapo Rais Samia ni mgeni rasmi .
Chongolo aliyeteuliwa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho jana Ijumaa, ametoa wito huo baada ya wafanyakazi walioshiriki maadhimisho hayo, kubeba mabango yenye ujumbe wa kudai ongezeko la mishahara.
Mabango hayo yalibeba kauli mbiu iliyosomeka “Maslahi bora, mishahara juu, kazi iendelee’.
“Leo mimi ni mara ya kwanza kusimama mbele ya halaiki hii, lakini si mgeni wa kazi za kusimama mbele ya watu, niseme sikukuu hii kwetu ni sehemu ya wajibu wa msingi sana kuzishiriki lakini pia kuhakikisha tunazifanya zijenge tabasamu kwa wafanyakazi,” amesema Chongolo
“Mimi sitasema mengi, nihitimishe kwa kusema, nina ujumbe wa kwaya moja ya Makongoro wanasema wanasubiri mama useme neno ili mioyo yao ipone. Nami sina shaka kwani ilani imeahidi masilahi bora ya watumishi, sina shaka kwa hilo ule ujumbe wa TUCTA (Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi Tanzania), mliofikisha kwa kwaya utafika,” amesema huku akishangiliwa.
Leave a comment