VYAMA vya wafanyakazi Mkoa wa Dodoma, wameiomba Serikali kuona uwezekano wa kuongeza mishahara kama inavyotakiwa kisheria. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Wametoa ombi hilo, leo Jumamosi, tarehe 1 Mei 2021, wakati wa maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Mei Mosi yaliyofanyika kimkoa katika uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.
Kauli mbiu ya maadhimisho ya Mei Mosi 2021 ni; Maslahi bora, mishahara juu, kazi iendelee.
Lizz Msechu, mwenyekiti Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Mkoa wa Dodoma amesema, kitendo cha wafanyakazi kutopandishiwa mishahara yao kwa kipindi cha miaka zaidi ya mitano, kinawafanya wafanyakazi kuishi maisha mabaya.
“Tunaomba serikali ione umuhimu wa kurejesha utaratibu wa kuongeza nyongeza za mishahara ili kuwe za kuwafanya wafanyakazi kuweza kuishi maisha ambayo yatakuwa na unafuu”amesema Msechu.
Pia, amesema wafanyakazi wanaiomba serikali kuona namna ya kubadili ulipaji wa kodi kwani watumishi wanajikuta wakilipa kodi mara mbili kwa maana ya kulipa kodi moja kwa moja inayokatwa kwenye mshahara na kulipa kodi wanapokwenda kununua bidhaa.
Katika hatua nyingine, amesema baadhi ya waajiri wamekuwa hawataki kuanzishwa kwa mabaraza ya kazi jambo ambalo linakinzana na utaratibu.
Akizungumzia kuhusu mafao ya wastaafu, Msechu amesema ni changamoto kubwa kwa kuwacheleweshea mafao yao wastaafu mafao tao.
Dk. Binirithi Mahenge, mkuu wa Mkoa wa Dodoma akijibu maombi hayo ya wafanyakazi amewaagiza waajiri wote kuhakikisha wanaanzisha mabaraza ya wafanyakazi katika sehemu za kazi.
Mbali na hilo, ameziagiza taasisi zote zinazotoa mafao ya wastaafu kuhamikisha wanatoa mafao kwa wakati badala ya kuwacheleweshea mafao yao.
Leave a comment