SERIKALI na jamii wametakiwa kuhakikisha wanatenga bajeti yenye mlengo wa kijinsia, ili kutokomeza ukatili wa kijinsia. Anaandika Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Rai hiyo imetolewa mkoani Dar es Salaam leo Jumatatu tarehe 16 Machi 2021, na washiriki wa warsha ya ujenzi wa nguvu za pamoja katika kuwezesha bajeti yenye mlengo wa kijinsia ili kuboresha maisha ya wanawake na watoto.
Akizungumza katika warsha hiyo Eduward Laiser, Diwani wa Kata ya Saranga amesema “uwezeshaji wa kiuchumi lazima tuuangalia kuanzia ngazi ya familia. Wanawake na wasichana wana uhitaji wa kuwezeshwa kupitia bajeti ili kuleta ulinzi.
“Sisi Kata ya Saranga wiki ijayo tunatarajia kusajili chama cha ushirika kwa wakazi wa Kata ya Saranga, ambacho kitagusa wajasiliamali wadogo hasa wanawake. Ushirika ukiwa imara hata ukatili utapungua,” amesema Laiser.
Liberatha Samson, Diwani wa Viti Maalum wa Kata ya Saranga amesema, bajeti huanzia chini, hivyo jamii inapowajengea uwezo kinamama, maana yake inasaidia bajeti kuu kuwa na mlengo wa kijinsia.
Anjela Mfinanga, Mwenyekiti wa Kituo cha Saranga amesema, lengo kuu la kituo ni kuwa chachu kwa wanajamii kujitafakari, kupata hamasa ya kushiriki na kuyashirikisha makundi yote yaliyo achwa nyuma katika maendeleo ikiwemo upatikanaji wa elimu, afya, maji na ushiriki katika njia za kiuchumi.
Hellen Urio, Mratibu wa Miradi kutoka Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), ambao ndio waandaaji wa warsha hiyo amesema, shirika hilo limefanya uraghibishi wa suala la bajeti kwa mrengo wa kijinsia, ambapo imesaidia kuamsha ari ya jamii kuamkuka na kuibua, kuchambua na kutekeleza ili kuleta mabadiliko pale walipo kwa kutumia rasilimali zilizopo.
“Kuanzia mwaka 2010, shirika likianza kutumia utaratibu wa vituo vya taarifa na maarifa ambavyo ni taasisi za kijamii katika ngazi ya kata.
“Mabadiliko mengi yamepatikana baada ya wananchi kujenga nguvu za pamoja na Halmashauri zao,” amesema Urio.
Leave a comment