KUELEKEA mchezo wao dhidi ya Namungo FC, kocha wa kikosi cha Pyramids FC, Rodolfo Arrubarrena pamoja na nahodha wake, Abdallah El Said wamejitanabaisha kuwa wamekuja Tanzania kuchukua pointi tatu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo wa Kombe la Shirikisho Afrika wa Kundi D, utachezwa kesho tarehe 17 Machi, 2021 majira ya saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
Akiongea kwenye mkutano wa waandishi wa habari hii leo, jijini Dar es Salaam kocha wa Pyramids, Arrubarrena, alisema kuwa wamejikita kwenye mchezo huo kwa ajili ya kuchukua pointi tatu.
“Tumejiandaa kwa mchezo huo na lengo ni kuchukua pointi tatu na wachezaji wapo tayari kwa ajili ya mchezo,” alisema kocha huyo.
Kwa upande wa nahodha, Abdallah El Said, amesema kuwa wamekuja hapa kuchukua pointi tatu licha ya kujua kwamba timu nyingi za Tanzania zinacheza mpira mzuri na haitakuwa mechi rahisi.
“Tumekuja hapa kuchukua alama tatu na najua timu nyingi za Tanzania zinacheza mpira mzuri, najua haitakuwa mchezo rahisi na tutafanya kila lililowezekana kuondoka na alama tatu,” alisema Nahodha huyo.
Huu utakuwa mchezo muhimu kwa Namungo kwenye kundi hilo, kutokana na kupoteza katika mchezo wa kwanza dhidi ya Raja Casablanca uliofanyika nchini Morocco.
Namungo wanashika nafasi ya tatu kwenye kundi hilo huku akiwa hana pointi.
Leave a comment