Thursday , 2 May 2024
Home Kitengo Habari Kimataifa Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi afungwa jela
KimataifaTangulizi

Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi afungwa jela

Spread the love

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Daniel Ngoyi Mulunda, sasa yuko gerezani anakotumikia kifungo chake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Mulunda anatuhumiwa kutumia lugha za uchochezi zenye lengo la kuzusha uhasama kati ya watu wa Katanga na Kasai, wakati wa usomaji wa misa ya kumbukumbu ya rais wa zamani wa taifa hilo, Laurent- Désiré Kabila.

Kwa mujibu wa vyombo vya usalama, Ngoyi Mulunda ambaye ni mchungaji, alikamatwa katika mji wa Katanga, Lubumbashi, mara baada ya kumaliza kuendesha misa iliyowakusanya maelfu ya wananchi katika kanisa lake.

Rais Laurent Desire Kabila, aliuawa kwa kupigwa risasi na mlinzi wake, tarehe 16 Januari 2001, akiwa ofisini kwake, jijini Kinshasa.

Mulunda alikamatwa mapema wiki hii, akituhumiwa kutoa hotuba ya kuchochea chuki na kuhujumu mamlaka ya nchi kwa kutishia kulitenga jimbo la Katanga.

Katika mahubiri hayo, Mulunda alilenga kuaminisha waumini wake, kwamba kuna  ubaguzi mkubwa kati ya watu wa Katanga anakotoka Kabila na wazawa wa mkoa wa Kasai, anakotoka rais wa sasa, Felix Tshisekedi na hivyo, kutaka kulitenga jimbo hilo kutoka DRC.

Laurent Desire Kabila, Laurent Desire Kabila, anachukuliwa kama mkombozi wa pili wa taifa hilo baada ya kuuangusha utawala wa Mobutu Sese Seko, Kuku Ngbwendu wa Za Banga. Kesi ya mauaji ya Kabila, bado inasuasua mahakamani.

Felix Tshisekedi, Rais wa DR Congo

Hata hivyo, aliyedaiwa kuwa mtuhumiwa mkuu wa mauaji hayo, Kanali Eddy Kapend, ameachiwa huru hivi karibuni, pamoja na washirika wengine 20, baada ya kupata msamaha kutoka kwa Rais Tshisekedi.

Alipokuwa akishikilia wadhifa wa mwenyekiti wa tume ya uchaguzi ya Kongo (CENI), Mulunda alisaidia sana wizi wa kura katika chaguzi zilizomuweka mamlakani Rais Joseph Kabila.

Gazeti la Die Tageszeitung la Ujerumani, linaeleza kuwa mwizi huyo mkubwa wa kura nchini DRC, katika uchaguzi wa mwishoni mwa mwaka 2011, alimtangaza Kabila kuwa mshindi baada ya kupata asilimia 48.95 ya kura.

Die Tageszeitung linasema, ushindi huo haukutokana na kura za wafuasi wake, “bali kazi yote ilifanywa na mwenyekiti wake wa tume ya uchaguzi, Daniel Ngoyi Mulunda.”

Taarifa zinasema, maelfu ya kura za aliyekuwa kiongozi wa upinzani nchini Kongo, Etienne Tshisekedi, zilipotezwa au kuharibiwa.

Gazeti la Die Tageszetung linasema, mkasa wa Ngoyi Mulunda unaashiria mwanzo wa mchakato wa kisheria wa kuihukumu enzi ya Kabila katika Kongo.

Madai ya wizi wa kura katika chaguzi nyingi zinazofanyika barani Afrika yamekuwa mambo yanayozoeleka katika siku za karibuni, jambo ambalo wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema, kifungo dhidi ya mwenyekiti wa uchaguzi nchini DRC, kinaweza kuwa labda fundisho kwa wenzake.

Nchini Tanzania kwa mfano, taarifa zinasema, katika uchaguzi mkuu uliyopita, lundo la kura zilizokuwa zimeshapigwa kwa wagombea wa chama tawala – Chama Cha Mapinduzi (CCM) – zilikamatwa kwenye vituo vya kupigia kura.

Joseph Kabila, Rais wa zamani wa DR Congo

Aidha, baadhi ya wagombea wa upinzani, walienguliwa kinyume na maelekezo ya sheria za uchaguzi, huku baadhi ya wapigakura wakituhumiwa kutumia vitambulisho feki, kupigia kura.

Pamoja na mapungufu hayo, mamlaka iliyokuwa inasimamia uchaguzi huo, iliruhusu kuendelea na kwa zoezi la uchaguzi hadi mwisho.

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi Zanzibar, Jecha Salim Jecha, aliamuru kufuta uchaguzi na matokeo yake Visiwani.

Jecha alisema, aliamua kufuta uchaguzi huo, baada ya kugundua kuwa aliyekuwa mgombea urais Visiwani katika uchaguzi huo, kupitia Chama cha Wananchi (CUF), aliiba kura na hivyo kusababisha kuwapo kura 15,000 za ziada, nje ya zile zilizochapishwa.

Alitangaza kufuta uchaguzi huo, wakati baadhi ya wagombea uwakilishi, wakiwa tayari wametangazwa washindi na wamekabidhiwa vyeti vyao.

Kitendo cha Jecha kuamua kufuta uchaguzi, kilisababisha Maalim Seif na chama chake, kususia uchaguzi wa marudio wa Machi mwaka 2016.

Lakini wakati Jecha akitoa tuhuma hizo, baadhi ya wangalizi wa kimataifa, walidai kuwa mgombea huyo wa upinzani alikuwa ameshinda uchaguzi huo, na kwamba uchaguzi huo ulikuwa huru na haki.

Ripoti za waangalizi zilizoonyesha kuwa uchaguzi wa 25 Oktoba, Visiwani ulikuwa huru, ni pamoja na ile iliyotolewa na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya (SADEC), pamoja na Umoja wa Africa (AU).

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Chadema kumshtaki Rais Samia

Spread the loveCHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetishia kumfungulia kesi ya...

Habari za SiasaKimataifa

Mwanamke Rwanda ataka kupambana tena na Kagame

Spread the loveKIONGOZI wa kihistoria wa upinzani nchini Rwanda, Victoire Ingabire Umuhoza,...

Habari MchanganyikoKimataifa

Ruto amteua Kahariri kuwa mkuu wa majeshi

Spread the loveRAIS wa Kenya, William Ruto, amemteua Jenerali Charles Muriu Kahariri,...

Habari za SiasaTangulizi

Serikali yaanza msako wanaotoa mikopo kausha damu

Spread the loveSERIKALI imeanza kufuatilia watu, vikundi na taasisi zinazotoa kinyume cha...

error: Content is protected !!