ZAIDI ya wanachama 1,100 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kata ya Mwakizega, Uvinza mkoani Kigoma, wamerejesha kadi za chama hicho wakidai, mgombea wa chama cha DP aliiba kura za mgombea wao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kigoma … (endelea).
Wanachama hao wamewatuhumu viongozi wa kata hiyo kubariki rafu zilizofanywa na Patrick Bitaliho, mgombea wa DP na kusababisha mgombea wao Swabiru Mussa, kushindwa kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 20 Oktoba 2020. Kwenye kata hiyo Bitaliho alitangazwa mshindi.
Wanachama hao wameeleza, kwamba walikutana na viongozi wa chama katika kata yao na kuwataka wafuatilie hujuma hizo, lakini mpaka wanachukua uamuzi huo, hakuna hatua zozote zilizokuwa zimechukuliwa.
“Hatua ya mgombea wetu kufanyiwa mziengwe ili aangushwe imetuumiza wengi, viongozi nao hakufuatilia licha ya kuwapa taarifa hiyo,” amesema Hafsa Ramadhani, mwachama wa chama hicho aliyedai kurejesha kadi yake.
Juma Yassin amesema, amuamua kurejesha kadi yake ya uanachama kwa Katibu wa CCM wa Kata ili kuonesha namna alivyokasirishwa na hujuma, pia uzembe wa viongozi wa kata kufuatilia madai yao.
Mbano Gwemela, Katibu wa CCM Kata ya Mwakizega amesema, amepokea kadi zaidi ya 1,100 za waliokuwa wanachama wa chama chake kwa madai ya kukasirishwa na hujuma zilizofanyika kwenye uchaguzi mkuu.
“Hapa nilipo kuna kadi 360 kutoka Kijiji cha Katete na kadi 740 zinatoka katika Kijiji cha Mwakizega. Kwa kweli jambo hili linanipa wakati mgumu sana kukabiliana nalo na wanachama hawataki kuelewa lolote kwa sababu bado wana hasira,” alisema Gwemela.
Mgombea mwenyewe Swabiru amedai, aliibiwa kura zake na Bitaliho wa Chama cha DP na kwamba, amepanga kukata rufaa. Madai hayo yameelezwa kwamba baadhi ya vituo taa zilizimwa kwa makusudi, vituo vingine matokeo yalibadilishwa na kumpa ushindi mgombea wa DP.
Leave a comment