RAIS wa Tanzania, John Magufuli amesema, utumbuaji kwa watumishi wa umma wazembe, wala rushwa, wezi na wabadhirifu, utaendelea katika miaka mitano ijayo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Akizungumza kwenye Uzinduzi wa Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo Ijumaa tarehe 13 Novemba 2020, Rais Magufuli amesema, watumishi wezi, wabadhirifu bado wapo hivyo ataendelea kuwang’oa.
“Watumishi wazembe, wala rushwa, wezi, wala mali bado wapo. Miaka mitano ijayo tutawashughulikia, kwa kifupi niseme utumbuaji utaendelea,” amesema Rais Magufuli.
Amesema, katika miaka mitano ijayo, Serikali anayoiongoza itaimarisha nidhamu na utawala bora na kwamba, miaka mitano iliyopita jumla ya watumishi 33,555 waliadabishwa ikiwa ni katika hatua za kulinda nidhamu ya utumishi wa umma.
“Nitaendelea kuimarisha utawala bora, kusimamia nidhamu ya utumishi wa umma. Nitakabiliana na wizi, ufisadi na ubadhirifu wa mali za umma. Miaka mitano iliyopita watumishi 32,555 tuliwaadibisha na tukashika nafasi ya kwanza kati ya nchi 35 Afrika, nafasi ya 28 kati ya nchi 136 dunia kwa mujibu wa jukwaa la dunia (World Forum) 2019.
“Tutaendelea kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ili yaendane na utumishi wa Watanzania, watumishi wasiwe na wasiwasi wachape kazi. Miaka mitano ijayo, tumejipanga kuendeleaza jitihada za kukuza uchumi,” amesema.
Leave a comment