RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Magufuli amesema katika kipindi cha miaka mitano ijayo serikali itajitahidi kutenga kiasi cha fedha kwa ajili ya Timu za Taifa za Tanzania ili kuziwezesha katika maandalizi mbalimbali. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Magufuli ameyasema hayo leo tarehe 13 Novemba, 2020, wakati wa hotuba ya ufunguzi wa Bunge la 12 jijini Dodoma ambayo ilitoa dira ya uongozi wake katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Kwenye hotuba hiyo, Magufuli alisema kuwa katika kipindi cha miaka m itano ijayo Serikali itatenga kiasi kidogo cha fedha katika kuziandaa timu mbalimbali za Taifa na pia alitumia fursa hiyo kwa kuitakia heri Taifa Stars kwenye mchezo wake wa leo dhidi ya Tunisia.
“Tutaanza kutenga fedha kidogo kidogo kwa ajili ya kuzianda timu zetu za Taifa na katika hilo napenda kutumia fursa hii, kuitakia heri timu yetu ya Taifa kwenye mechi yao dhidi ya Tunisia hapo baadaye,” alisema Magufuli.
Aidha Rais Magufuli aliongezea kwa kumtakia heri bondia Mtanzania Hassan Mwakinyo ambaye anashuka ulingoni hapo baadaye, kupambana na bondia kutoka nchini Argentina kwenye pambano la raundi 12 la ubingwa wa mabara wa IBF.
“Na pia nataka kumtakia heri mwanamasumbwi wetu, Hassan Mwakinyo anayepambana leo, watanzania tunataka ushindi tumechoka kushindwa,” aliongezea Magufuli.
Pia kwa upande mwingine, Magufuli alisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano ijayo watajipanga kukuza sekta ya Sanaa, na utamaduni kwa kusimamia hati miliki ili kunifaika na kazi zao.
“Kwenye miaka mitano ijayo pia tutakuza sekta ya sanaa, michezo na utamaduni ambayo inakuwa kwa kasi kubwa saa, tutaikuza sekta hii husausan kusimamia masuala ya hati miliki ili kunufainika na kazi zao.
“Ninafarijika kwamba kuna wasanii ambao ni wabunge miongoni mwetu humu, tutauuhisha pia mfuko wa utamaduni wa sanaa ili kuwasaidia wasanii wetu ikiwemo kupata mafunzo na mikopo,” aliongezea Rais Magufuli.
Majira ya saa nne usiku timu ya Taifa itakuwa jijini Tunis kwenye mchezo wa Kundi J, kusaka tiketi ya kucheza michuano ya Kombe la Mataifa Afrika 2022 nchini Cameroon ambapo itamenyana na timu ya Taifa ya Tunisia.
Leave a comment