MABINGWA wa kihistoria nchini Tanzania, Yanga, imemtangaza Zlatko Krmpotic kuwa Kocha Mkuu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kocha huyo anakuja kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Luc Eymael raia wa Ubelgiji aliyetimuliwa tarehe 27 Julai 2020 kutokana na kutuhumiwa kutoa lugha zisizo za kiungwana.
Yanga imejikuta ikitua kwa raia huyo wa Serbia baada ya kushindwa kuelewana na Cedrick Kaze raia wa Burundi.
Kaze alikuwa awasili Tanzania leo Ijumaa tarehe 28 Agosti 2020 kuanza kibarua kipya ndani ya timu hiyo ya Jangwani, Dar es Salaam lakini akatoa udhuru na kutaka apewe wiki tatu zaidi ili kumaliza matatizo ya kifamilia yaliyokuwa yakimsibu.
Hata hivyo, Yanga haikukubaliana na ombi hilo na kuamua kutua kwa Krmpotic ambaye amehudumu kama kocha katika nchi 12 tofauti ikiwemo DR Congo katika timu ya TP Mazembe akiwa kocha msaidizi na kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Timu zingine alizozifundisha ni; APR ya Rwanda na Zesco ya Zambia na timu ya mwisho mwisho kuifundisha ni Polokwane City FC ya Afrika Kusini.
Krmpotic atakuwa akisaidiwa na kocha msaidizi, Juma Mwambusi ambaye ndiye anayekinoa kwa sasa.
Yanga inaendelea na sherehe za “Wiki ya Mwananchi’ ambayo kilele chake kitahitimishwa Jumapili tarehe 30 Agosti 2020 Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Siku hiyo, kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali akiwemo, Rajab Abdul Kahali maarufu Harmonize au ‘Konde Boy.’
Pia, kutakuwa na utambulisho wa wachezaji watakaotumika msimu wa 2020/21 na mwisho siku, itahitimishwa kwa mchezo wa kirafiki utakaochezwa dhidi ya Aigle Noir ya Burundi huku mgeni rasmi akiwa Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.
Leave a comment