WANACHAMA watatu wa chama cha NCCR-Mageuzi nchini Tanzania, watachuana kuwania kuteuliwa na chama hicho kugombea urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Miongoni mwa watia nia hao watakaouama kesho Ijumaa tarehe 7 Agosti 2020 katika mkutano mkuu utakaofanyika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam ni, Yeremia Kurwa Maganja, aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa chama cha ACT-Wazalendo.
Mkuu wa Idara ya Uenezi na Mahusiano ya Umma wa NCCR Mageuzi, Edward Simbeye amesema, Maganja atachuana na watia nia wengine ambao ni Peterson Mushenyera, Abubakari Juma.
Amesema kwa upande wa Zanzibar mtia nia mmoja ambaye amechukua fomu ni Haji Hamisi.
“Kesho tarehe 7 Agosti kutakuwa na kikao cha kufanya mchujo ili kupata jina moja moja, chama kitachagua wagombea urais Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema.
Aidha, Simbeye amesema, shughuli ya kuchukua fomu za kugombea ubunge na udiwani linakoma kesho tarehe 7 Agosti 2020 na tarehe 25 Agosti 2020 kitakuwa kikao cha mchujo wa wabunge na madiwani.
Kuhusu James Mbatia, mwenyekiti wa chama hicho kutochukua fomu ya urais Simbeye amesema, ni hiyari yake kuchukua ama kutochukua lakini waliochukua fomu wana vigezo vyote na vimejitosheleza kikatiba.
Hata hivyo, amesema NCCR-Mageu kipo radhi kushirikiana na chama chochote katika uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 chenye mlengo wa kuhitaji demokrasia na kuwa milango ipo wazi kwa yoyoye anayehitaji ushirika.
“Kwa hatua ya kwanza, kwakuwa kila chama kina lengo la kuchukua dola, tunaendelea na mchakato wa kupata wagombea kwasababu hatutavuka daraja la ushirikiano kama hatuna wagombea,” amesema Simbeye.
Leave a comment