AWAMU ya kwanza ya Ujenzi wa Mradi wa maji wa Jeti-Buza jijini Dar es Salaam inaendelea kwa kasi ambapo mtandao wa bomba la umbali wa Kilomita 7.5 umeshatandazwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Mradi huo unaojengwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kupitia fedha za ndani za mamlaka hiyo utahudumia wakazi wa maeneo ya Kiwalani, Vituka, Buza ,Machine namba 5 -Tandika na Mwanagati.
Wakiwa katika ziara ya kuangalia maendeleo ya mradi huo leo Alhamisi tarehe 6 Agosti 2020, Msimamizi wa mradi huo, Mhandisi John Romanus wa Dawasa amesema hadi sasa mradi huo umefikia asilimia 85 hadi kukamilika kwake.
“Kazi ya ulazaji bomba imekamilika kwa asilimia 100 ambapo bomba la inch 16 limeshalazwa kwa umbali wa kilomita 7 kuanzia eneo la Jet corner mpaka njia panda ya Buza” amesema Mhandisi Romanus.
Amesema kazi zilizobaki ni uwekaji wa mfumo wa kusafisha bomba (washout) pamoja kujengea mfumo wa kutoa hewa kwenye bomba (airvalve).
“Kazi hizi zinategemea kumalizika ndani ya miezi miwili kuanzia sasa hivyo kufanya mradi huu kufikia hatua za mwisho za utekelezaji wake,” amesema Mhandisi Romanus
Kwa upande wake, Meneja mawasiliano Dawasa, Everlasting Lyaro ametoa wito kwa wananchi wa maeneo yatakayohudumiwa na mradi, kupata taarifa sahihi kwa watendaji wa Kata na mitaa yao ili kupata uelewa wa pamoja wa mradi na kuepuka taarifa zisizo sahihi.
“Tunajua shauku kubwa ya wananchi wa huku wanaosubiri kuhudumiwa na Dawasa pindi mradi utakapokamilika.”
“Nitoe rai kwa wananchi kutembelea ofisi za watendaji wa kata na mitaa yao ili kupata taarifa sahihi za mradi, utaratibu wa kupata huduma pindi mradi utakapokamilika na taarifa nyingine muhimu za Dawasa,” amesema Everlasting.
Kuhusu chimbuko la mradi huo ni baada ya kukamilika kwa upanuzi wa Mtambo wa Ruvu Juu uliopelekea ongezeko la Maji
Everlasting amesema, Dawasa walianza ujenzi wa mradi huo baada ya upanuzi wa mtambo wa Ruvu juu uliopelekea kuongeza kwa kiwango cha uzalishaji maji kutoka mita za ujazo 90,000 hadi kufikia mita za ujazo 180,000 .
Amesema, kutokana na ongezeko hilo, Dawasa wakaamua kuanzisha mradi mkubwa wa mtandao wa maji kwa maeneo ya Dar es Salaam ya kusini.
“Lengo la mradi wa maji Jet-Lumo ni kuhudumia wakazi wa maeneo ya Kiwalani, Vituka, Buza, mashine namba 5-Tandika na Mwanagati ila kwa sasa tumeanza na awamu ya kwanza, ambayo inaenda kukamilika,” amesema Everlasting
“Mwaka wa fedha 2019/20 Dawasa kupitia mapato yake ya ndani ilitenga kiasi cha Sh.2.2 bilioni kwa ajili ya mradi huu ambapo kukamilika kwake utahudumia wakazi takribani 173,810 wa kata za Yombo Vituka hadi Buza” alisema Lyaro
Naye mtendaji wa mtaa wa Magogoni kata ya Yombo Vituka, Upendo Sinawi ameishukuru Dawasa kwa kuwalatea mradi mkubwa wa maji utakaoenda kuondoa adha ya kutumia maji ya visima ambavyo vingi havikuwa salama kwa wananchi.
“Kwa miaka mingi eneo hili huduma ya Majisafi tunaipata kupitia visima vya watu binafsi au jumuiya ambavyo maji yake yanaweza kuwa na chumvi nyingi au yasiwe salama kwa matumizi ya binadamu.”
“Hivyo mradi huu wa maji ni mkombozi mkubwa kwa sisi viongozi wa wananchi kwani wananchi wetu watapata maji safi na salama kutoka Dawasa” amesema mtendaji Sinawi
Baada ya kukamilika kwa awamu ya kwanza ya mradi, uendelezaji wa mradi kwa awamu ya pili utakuwa katika maeneo ya mashine namba 5-Tandika, Mwanagati,Kiwalani na baadae hadi Gongo la Mboto Jijini Dar es salaam.
Leave a comment