CHAMA cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kimelaani kauli zinazotolewa na baadhi ya viongozi wa umma, zinazochochea watu kuchukua sheria mikononi dhidi ya watuhumiwa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Akizungumza katika mkutano mkuu wa nusu mwaka wa chama hicho, uliofanyika leo tarehe 7 Septemba 2019 jijini Arusha, Dk. Rugemeleza Nshala, Rais wa TLS ameitaka serikali kuwachukulia hatua viongozi wanaotoa kauli hizo.
Dk. Nshala ameeleza kuwa, ni kinyume na sheria kwa kiongozi yeyote kutoa kauli ya kuruhusu watu kupigwa, kuvunjwa miguu au kuuawa pindi wanapokutwa na makosa.
“Ni kinyume cha katiba ya nchi kwa kiongozi yoyote kutoa kauli ya kuruhusu watu kupiga na kuvunjwa au hata kuuwawa pindi wanapokutwa na makosa. Ofisi zenye mamlaka lazima ziwachukulie hatua viongozi wote wanaohusika na matamshi haya,” amesema Dk. Nshala.
Hivi karibuni, Sara Msafiri, Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni alitangaza zoezi la kuwakamata, kuwapiga na kuwavunja miguu watu watakaobainika kuhusika na wizi wa vifaa vya magari unaofanyika usiku.
Msafiri alisema wezi hao wakikamatwa huachiwa kwa dhamana mahakamani, na kuendelea na udokozi huo unaofanya wengine kuwa masikini badala ya kujihusisha na shughuli halali za uzalishaji kwa ajili ya kujipatia kipato.
Leave a comment