MAJERUHI wanne kati ya 25 wa ajali ya moto iliyotokea mkoani Morogoro waliokuwa wanaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wamepoteza maisha jana tarehe 16 Agosti 2019. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
MNH ilipokea majeruhi 46 wa ajali hiyo iliyotokea tarehe 10 Agosti mwaka huu maeneo ya Msamvu mkoani Morogoro, waliotokea katika hospitali ya rufaa ya mkoani humo ambapo kwa sasa walio hai ni 21, na waliopoteza maisha 25.
Tarehe 14 Agosti 2019 walifariki dunia majeruhi 14, wakati majeruhi 7 wakipoteza maisha Usiku wa kuamkia Agosti 15 huku wengine wanne walifariki dunia jana. Kufuatia vifo hivyo, idadi kamili ya vifo vilivyotokana na ajali hiyo imefikia 93.
Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto jana alitembelea hospitalini hapo kwa ajili ya kuwaona majeruhi hao, na kueleza kwamba madaktari na wauguzi wanafanya kila njia kunusuru maisha yao.
Aidha, Ummy aliagiza Kitengo Maalum cha Kuhudumia Wagonjwa wa ajali za moto kianzishwe MNH.
Dk. Juma Mfinanga, Mkuu wa Idara ya Kitengo cha Dharula MNH amesema majeruhi waliobaki wamewekwa katika Chumba cha Uangalizi Maalumu (ICU) ili kuhudumiwa kwa umakini zaidi.
Leave a comment