NCHI ya Palestina imetoa pole kwa serikali ya Tanzania kufuatia vifo vya watu 93 vilivyotokea katika ajali ya mlipuko wa tenki la mafuta mkoani Morogoro tarehe 10 Agosti 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Salamu hizo za pole zimetolewa na Dk. Riad Malki Waziri wa Mambo ya nje wa Palestina kupitia barua aliyomwandikia Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana tarehe 16 Agosti 2019 na Kitengo cha Mawasiliano cha Ubalozi wa Palestina hapa nchini, Dk. Malki ameeleza kuhuzunishwa na tukio hilo, huku akisema kwamba serikali na raia wa Palestina wanawaombea majeruhi wote wapone haraka pamoja na marehemu wapumzike kwa amani.
“Nimepokea kwa huzuni kubwa habari za kifo na majeruhi ya raia kutokana na tukio la mlipuko wa tanki la mafuta lililotokea mkoa wa Morogoro. Kwa niaba ya serikali na watu wa nchi ya Palestina, ningependa kutoa salamu zangu za pole kwa watu na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mawazo yetu na sala ziko pamoja na familia za waathirika wa mlipuko huo na kuwaombea majeruhi wapone haraka,” inaeleza sehemu ya barua ya Dk. Malki kwa Prof. Kabudi.
Leave a comment