MBUNGE wa Bunda Mjini (CHADEMA), Esther Bulaya, “ameliamsha dude.” Amesema, serikali imekopa mabilioni ya shilingi mashirika ya umma, ikiwamo Jeshi la Kujenga la taifa (JKT). Anaripoti Mwandishi Wetu kutoka Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni mjini Dodoma, leo Jumamosi, tarehe 2 Februari, Bulaya amesema, mashirika na mifuko ya hifadhi ya jamii, inadai serikali zaidi ya Sh. 10 trilioni, huku baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakidaiwa zaidi ya Sh. 3.2 trilioni kutokana na mikopo iliyochukua JKT.
“Lipeni madeni haya, ili mashirika yetu ya umma yaweze kupata mtaji na kuweza kujiendesha. Acheni kugagaa. Achene kuleta porojo,” alieleza Bulaya.
Huku akionyeshea mkono upande walioketi wabunge wa CCM, Bulaya alisema, kuna ubadhilifu mkubwa ndani ya serikali na ndani ya mashirika hayo ya umma, kutokana na kuwapo mipango mibaya ya serikali.
Bulaya alitoa kauli hiyo, wakati wa mjadala wa taarifa ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma. Taarifa ya Kamati ya Mitaji iliwasilishwa bungeni na Dk. Raphael Chegeni, mwenyekiti wa kamati hiyo na mbunge wa Busega mkoani Simiyu.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma, mashirika kadhaa ya serikali yanaidai serikali; na au kudaiwa na mashirika mengine.
Miongoni mwa mashirika hayo, ni pamoja na Mamlaka ya Maji Safi na Majitaka jijini Dar es Salaam (DAWASA); Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Magereza.
Wadai wakubwa wa mashirika hayo, DAWASA inayodaiwa Sh. 6 bilioni, jeshi la Magereza linalodaiwa Sh. 7 bilioni, JWTZ linalodaiwa Sh. 8 bilioni na hospitali ya Muhimbili inayodaiwa zaidi ya Sh. 5 bilioni.
Leave a comment