BAADA ya timu zote mbili kupoteza michezo yao siku ya Jumamosi wakiwa ugenini, zote zimerudi jijini Dar es Salaam kujiandaa na michuano ya kombe la SportPesa inayotarajia kuanza kutimua vumbi siku ya kesho 22 Januari, 2019 katika uwanja wa Taifa. Anaripoti Kelvin Mwaipungu… (endelea).
Yanga ilipoteza mchezo kwa mara ya kwanza kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara mbele ya Stand United ‘Chama la Wana’ baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0, huku Simba wakipokea kipigo kizito cha bao 5-0 kutoka kwa AS Vital ya Congo katika mchezo wa klabu bingwa barani Afrika hatua ya makundi.
Wawakilishi haio wa Tanzania wanatarajia kuanza kutupa karata zao siku ya kesho ambapo Yanga atamenyana dhidi ya KK Sharks kutoka nchini Kenya majira ya saa 10 jioni, huku Simba watashuka dimbani siku ya Jumatano kuwakabili AFC Leopards kutoka Kenya.
Ikumbukwe bingwa wa michuano hiyo atapata zawadi ya fedha, kombe sambamba na kucheza na klabu ya Everton inayoshiriki Ligi Kuu England kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa mashindano.
Timu zingine zitakazo shiriki michuano hiyo ni pamoja na bingwa mtetezi wa michuano hiyo mara mbili Gol Mahia kutoka Kenya, Bandari FC na Singida United ya Tanzania, Mbao FC ya Tanzania na Kaliabangi ya Kenya.
Leave a comment