MJUMBE wa Baraza Kuu la Uongozi la CUF Taifa, Abdallah Khatau leo amefikisha siku ya tano akiwa rumande huku polisi wakigoma kumpa dhamana. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Licha ya kumnyima dhamana, Polisi wa Kituo cha Polisi cha Masasi mkoani Mtwara wamegomea ndugu zake kumuona Khatau.
Kwa mujibu wa ndugu wa karibu wa Khatau, Ebrahim Issally kupitia ukurasa wake wa Twitter jana tarehe 18 Januari 2019 aliandika kuwa, polisi hawajaeleza sababu za kukamatwa kwa Khatau pia wamegoma kuruhusu kumuona ndugu yao.
Naibu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano na Umma CUF, Mbarala Maharagande amesema, hadi leo tarehe 19 Januari 2019, Khatau bado anashikiliwa na Jeshi la Polisi na kwamba, chama chake kinaendelea na jitihada za kushughulikia dhamana yake.
Alipoulizwa sababu za kukamatwa Khatau, Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Blasius Chatanda alidai hana taarifa za kukamatwa kwa Khatau.
Pamoja na hivyo Kamanda Chatanda amesema, sio jambo rahisi kwa polisi kumkamata mtuhumiwa bila kueleza sababu.
Kamanda Chatanda ameshauri ndugu wa Khatau kwenda kwa Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Masasi (OCD), ili kujua sababu zilizopelekea Khatau kushikiliwa na Jeshi la Polisi.
“Sina taarifa hizo, ndio nasikia kutoka kwako, ila nitafuatilia taarifa hizo. Lakini haiwezekani polisi wamkamate bila ya kumwambia kosa. Kwa msaada wakamuone OCD,” amesema Kamanda Chatanda.
Khatau ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini CUF, alikamatwa tarehe 15 Januari 2019 akiwa nyumbani kwake wilayani Masasi.
Leave a comment