RAIS Joseph Kamembe Kabila, amegomea wito wa Muungano wa Afrika (AU), wanaotaka kucheleweshwa kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi wa rais nchini mwake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Muungano wa Afrika unasema, unatilia mashaka uadilifu wa matokeo yaliyotangazwa wiki mbili zilizopita nchini humo na ambayo yamempatia ushindi, kiongozi wa upinzani, Felix Tshisekedi.
Msemaji wa serikali ya Kongo, Lambert Mende amesema, Mahakama ya Kikatiba ni taasisi huru na hakuna mtu yeyote mwenye haki ya kuielekeza.
Uamuzi wa AU kuingilia hali ya kisiasa nchini humo, inatokana na hatua ya kiongozi mwingine wa upinzani, Martin Fayulu kupinga matokeo hayo.
Tayari Fayulu ametinga mahakamani kupinga matokeo hayo. Anaiomba mahakama kufutilia mbali matokeo hayo; na kudai kuwa ndiye aliyeshinda uchaguzi huo.
Muungano wa Afrika unasema kuwa mwenyekiti wake, Rais Paul Kagame (Rwanda) na viongozi wengine wataelekea Kinshasa kutafuta suluhu ya mgogoro huo.
Msemaji huyo wa serikali (Mende) anasema, ujumbe wa rais Kagame unakaribishwa nchini mwake, lakini anasisitiza kuwa matokeo hayo ya baada ya uchaguzi hayatabadilishwa.
“Rais mteule Felix Tshisekedi, ataweza kuapishwa ndani ya muda mchache kutoka sasa, iwapo Mahakama itamthibitisha. Hatutasikiliza matakwa ya watu wengine,” ameeleza Mende.
AU unaonuia kuhimiza umoja na demokrasia, unasema una “shaka kubwa” na matokeo ya awali yaliotangazwa wiki iliyopita. Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kutangazwa leo Ijumaa.
Kumezushwa maswali mengi kuhusu uhakika wa matokeo hayo huku kukiwepo shutuma kwamba Tshisekedi anapanga mpango wa kugawana madaraka na rais anayeondoka Joseph Kabila.
Baadhi ya viongozi katika Muungano wa Afrika na serikali walikutana katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa jana Alhamisi na kutoa tamko kuhusu uchaguzi huo wa Desemba 30 unaopingwa pakubwa.
“Kumekuwa na shaka kubwa kuhusu namna matokeo ya awali yalivyokusanywa, kama ilivyotangazwa na tume huru ya kitaifa ya uchaguzi kwa kura zilizopigwa,” taarifa ya muungano huo imesema.
“Kadhalika, AU imetaka kuahirishwa kutangazwa kwa matokeo ya mwisho ya uchaguzi mkuu huo,” iliongeza taarifa.
Fayulu anatuhumu kwamba mshindi wa muda bwana Tshisekedi alikubaliana na rais anayeondoka Joseph Kabila.
Kabila amehudumu kwa miaka 18 na matokeo, iwapo yatathibitishwa, yataidhinisha ukabidhi wa kwanza wa uongozi kwa mpangilio tangu taifa hilo lipate uhuru kutoka kwa Ubelgiji mnamo 1960.
Tume ya uchaguzi imesema Tshisekedi alishinda 38.5% ya kura, ikilinganishwa na 34.7% alizoshinda Fayulu. Mgombea wa muungano wa serikali Emmanuel Shadary alijizolea 23.8%.
Matokeo hayo yanatarajiwa kutangazwa kama ni mapema sana leo, na wataalamu wanasema kuna uwezekano wa matokeo matatu.
Leave a comment