CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimezidi kuogopa kivuli cha Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), baada ya kutimua wagombea wa uenyekiti wa wilaya ambazo Chadema kimeshinda ubunge, anaandika Hamisi Mguta.
CCM kimefuta majina ya wanachama waliopitishwa kugombea uenyekiti katika wilaya za Hai, Moshi mjini na Siha ambako Chadema kilishinda ubunge mwaka 2015.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Hamprey Polepole ametangaza hayo leo, baada ya kumalizika kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM kilichofanyika jijini Dar es Salaam.
Polepole amesema wagombea wote waliofutwa wamebainika kuwa walikuwa na viashiria vya kuhatarisha uhai wa chama pamoja na kasoro mbalimbali.
Aidha, katika wilaya ya Musoma vijijini uchaguzi wa ngazi ya mwenyekiti wa wilaya pamoja na jumuiya zingine utafanyika baada ya chama kutangaza.
Wale ambao watapewa dhamana kwenye ngazi ya wilaya na wana nafasi zingine za uongozi watapaswa kuachia nafasi zao za awali."-@hpolepole
— Chama Cha Mapinduzi (@ccm_tanzania) September 30, 2017
Hatua hiyo imefikiwa baada ya CCM kuamua kupanua wigo na kugawa wilaya za Musoma mjini na Musoma vijijini.
Amesema kila mwanachama wa CCM anatakiwa muda wote kuzingatia maadili, kanuni na taratibu zote za chama na kwamba atakayekwenda kinyume chake atafukuzwa uanachama.
CCM kimetangaza kwamba hakuna mwanachama atakayeshikilia nafasi mbili kwa wakati mmoja na kwamba hilo halina mjadala lazima mtu mmoja awe na kofia moja.
Polepole akizungumzia upande wa Zanzibar, amesema wamepata taarifa kuna watu wameanza kampeni kwa ajili ya kupata urais visiwani humo kabla ya wakati wake kufika na kwamba chama kimewaonya.
Kimewataka kuacha mara moja mpango huo vinginevyo wakibainika kwa ushahidi watatimuliwa ndani ya chama.
Kwa upande wa wanachama ambao hawakuridhika na maamuzi ya vikao kwa ngazi waliogombea wametakiwa kufkata rufaa ngazi ya juu yake ili kuhakikisha haki inapatikana.
Amesema kila mtu atapata haki yake kwa kufuata tataribu zilizowekwa na chama kupitia vikao. Chama cha Mapinduzi (CCM) katika kikao hicho kimepitisha majina ya wenyeviti 161 wa wilaya za Tanzania Bara.
Leave a comment