SERIKALI mkoani Morogoro kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imevifungia vituo vinne vya kuuza mafuta, kwa kosa la kukiuka agizo la Rais John Magufuli la kuwataka wafanyabiashara kutumia mashine za EFDs, anaandika Christina Haule.
Akizungumza wakati akifunga vituo vitatu vya mafuta vya Lake Oil Mkuu wa mkoa wa Morogoro Dk. Kebwe Steven Kebwe alisema, amelazimika kuvifungia kutokana na kukiuka agizo la Serikali na kuzuia mapato ya Serikali.
Aidha, Dk. Kebwe alimtaka mmiliki wa vituo hivyo kutochukua hatua zozote za ujanja ujanja na kufungua mashine hizo kwa nia ya kuuza mafuta na kwamba akibainika atashtakiwa kama mhujumu uchumi.
Naye Meneja wa kituo cha Lake Oil cha Msamvu Manispaa ya Morogoro, Amri Saidi alisema, anashangazwa na kitendo cha TRA kufunga kituo hicho kwa mtu anayehusika kulipia mashine hizo alikuwa yupo ofisi za mamalaka hiyo.
Saidi amesema, wao wana vituo 70 nchi nzima ambapo wanatumia wakala mmoja kukamilisha kufunga mashine hizo huku wakiwa tayari wameshaweka stendi za kufungia mashine hizo kwenye kituo chao.
Leave a comment