MFULULIZO wa mauaji yanayoendelea wilayani Kibiti Mkoa wa Pwani yamewatikisa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuombaratiba ya leo ya shughuli za Bunge iahirishwe ili kujadili jambo hilo kama jambo la dharura, anaandika Dany Tibason.
Mchungaji Peter Msigwa Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), katika muongozo wake leo bungeni amemuomba Dk. Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge akubali Bunge lisimamishe shughuli zote ili kujadili kwa dharura mauaji yanayoendelea wilayani Kibiti.
“Tuliwahi kuhoji hapa bungeni kuhusu mauaji ya Kibiti, lakini Serikali ilisema tuipe muda na kila Serikali inapotoa matangazo ya kusema imejipanga, ndipo mauaji yanapozidi kutokea, sisi kama wabunge tuna wajibu wa kuisimamia Serikali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha ulinzi wa raia,” amesema Msigwa.
Hoja ya Msigwa ilionekana kuungwa mkono na wabunge wengi lakini Dk. Tulia akijibu muongozo huo amesema hawezi kusimamisha shughuli za Bunge kujadili kwa dharura mauaji ya raia na askari polisi wilayani Kibiti kwani Serikali inafuata utaratibu wa kisheria kushughulikia jambo hilo.
“Kwa mujibu wa kanuni ya 47 (4), nimeridhika kwamba Serikali inafuata utaratibu uliopo wa kisheria wa kushughulikia jambo hili na hata kama tukitaka kulijadili, bado hata sisi tutatakiwa kujadili sheria zinasema nini na Serikali inapaswa kufanya nini.
“Mheshimiwa Msigwa analitaka Bunge liahirishe shughuli zake ili lijadili jambo hili na kama jambo la dharura lakini kanuni ya 48 inaweka masharti ya jumla kuhusu jambo la dharura, inasema dharura ni lazima iwe imethibitishwa ndipo Bunge lisitishe shughuli zake ili kulijadili,” amesema.
Mch. Msigwa ameomba suala la hali ya usalama Kibiti kujadiliwa bungeni ikiwa ni siku moja tu baada ya askari wawili wa kikosi cha usalama barabarani kuuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana wilayani humo wakati wakitekeleza wajibu wao.
Leave a comment