NUSU ya maiti 400 zilizotokana na maporomoko ya udongo na mafuriko nje ya mji wa Freetown tayari zimezikwa, anaandika Hamisi Mguta.
Serikali nchini humo ilisema mazishi ya pamoja yangeahirishwa hadi leo ili kutoa fursa kwa ndugu na jamaa kutambua miili ya maiti ya waathirika.
Lakini mkuu wa wataalamu wa magonjwa kutoka mjini Freetown ameliambia shirika la habari la BBC kuwa baadhi ya mazishi yalikuwa yamekwishafanyika.
Imefahamika kuwa mazishi hayo yamehusisha miili ambayo tayari ilitambuliwa au ilikuwa imeharibika kabisa.
Watu wapatao 600 mpaka sasa hawajulikani walipo huku Rais wa Sierra Leone ametangaza siku saba za maombolezi.
Nathaniel Williams ni daktari katika hospitali kuu ya Connaught, iliyopo Freetown, anasema hivi sasa kuna tahadhari kubwa ya kutokea magonjwa ya milipuko kama vile kipindupindu hivyo sasa kunahitajika madawa na vyakula, kwa wale walioathirika.
Hata hivyo, Umoja wa Mataifa nchini humo umesema tayari umeweka mikakati ya kuweza kukabiliana na magonjwa ya milipuko iwapo yatatokea.
Leave a comment