RUHUSA kwa raia wa Cuba kuingia Marekani bila na kibali cha kusafiria na kuishi, yaani ‘viza’ sasa imekwisha. Wale walioingia nchini humo kinyume na utaratibu unaolingana na wahamiaji wa nchi zingine wanapaswa kuondoka mara moja, anaandika Wolfram Mwalongo.
Rais anayemaliza muda wake Barack Obama amefikia uamuzi huo kutokana na wimbi kubwa la wahamiaji kutoka Cuba.
Wachambuzi wa masuala ya kidiplomasia wanahofia kuwa huenda hatua hiyo ikaweka rehani uhusiano baina ya mataifa hayo mawili.
Kwa upande wa pili wafuasi wa Rais mteule Donald Trump wamefurahishwa na hatua hiyo wakiamini ni mwanzo wa utekelezaji wa sera za kiongozi huyo mwenye azma ya kujenga ukuta mapakani mwa Marekani na Mexico.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Marekani Alhamis ya wiki hii imesema kuwa sheria iliyokuwepo na ikijulikana kwa jina maarufu la “Wet foot, Dry foot” imefutwa ikiwa ni miongoni mwa mabadiliko kadhaa ambayo yameendelea kufanyika wakati huu ambao Obama amebakiza siku tano tu za kukaa Ikulu.
“Rai kafanya jambo muhimu lakini pia Cuba imekuwa ikihitaji kwa zaidi ya muongo sasa, kutokana na wananchi wao wengi kukimbia kisiwa chao. Iwe kwa uzuri au kwa ubaya lakini kwa sasa raia wa Cuba watakuwa wakiingia Marekani kwa kufuata taratibu kama wahamiaji wengine,” amesema Gustavo Arnavat, mtumishi wa zamani wa Rais Obama.
Mwaka 2015 Rais Obama alitangaza kuiondolea Cuba vikwazo vilivyowekwa na Marekani kwa zaidi ya miaka 50 iliyopita, kutokana na uhasama uliokuwepo baina ya mataifa hayo.
Hali hiyo ilitokana na msimamo wa Rais Fidel Castro wa Cuba kugomea mataifa yenye hulka ya ubeberu.
Leave a comment