SERIKALI inadaiwa jumla ya Sh. 254.1 milioni na walimu wa Halmashauri ya Bahi mkoani Dodoma, ikiwa ni malimbikizo ya mishahara na posho, anaandika Dany Tibason.
Kutokana na madeni hayo, halmashauri hiyo imeshindwa kuwasafirisha walimu wastaafu 28 kurudi kwao baada ya kustaafu, kwani wastaafu hao wanaidai serikali jumla ya Sh. 42.8 milioni.
Akisoma risala wakati wa hafla ya kuwaaga walimu wastaafu Anna Senge, Katibu wa Chama cha Walimu
(CWT) Wilaya ya Bahi, amesema walimu wa wilaya hiyo wanakabiliwa na changamoto lukuki.
“Walimu wa wilaya hii wanafanya kazi katika mazingira magumu pamoja na kucheleweshewa stahiki zao.
Hata upatikanaji wa stakabadhi za malipo ya mishahara umekuwa mgumu jambo linalowanyima walimu haki ya kudai malimbikizo yao ya mishahara,” amesema.
Amedai kuwa walimu 346 waliotarajia kupanda vyeo kwa mwaka 2016/2017 hawajapandishwa na pia walimu 220 waliopandishwa vyeo mwezi Januari 2016 mpaka sasa hawajarekebishwa madaraja ya mishahara yao na hivyo wanafanya kazi kwa kukata tamaa.
Katika hatua nyingine amesema mkurugenzi wa halmashauri ya Bahi ameshindwa kuwalipa hata zawadi zao walimu watatu hodari ambao walitangazwa wakati wa siku ya Mei Mosi mwaka jana. Walistahili kupewa zawadi ya jumla ya Sh. 1.5 milioni.
Kwa upande wake Hamisi Nakomolwa mwalimu mstaafu wa Shule ya Msingi Kigwe, amesema serikali imekuwa ikichelewesha mafao ya wastaafu na hivyo kuwasababishia maisha magumu huku akitolea mfano yeye aiyestaafu Agosti mwaka jana lakini hadi leo hajalipwa mafao yake wala fedha ya kumsafirisha kutoka kituo chake cha kazi.
Leave a comment