MAREKANI imetishia kusitisha misaada kwa viongozi wa Sudan Kusini endapo hawatashiriki katika mazungumzo ya ngazi ya juu na kushindwa kuheshimu muda wa mwisho wa kusitisha mapigano, anaandika Catherine Kayombo.
Msimamo huo umetolewa na Naibu Balozi wa Marekani katika umoja wa mataifa, Michele Sison, na kusema kwamba mazungumzo hayo yaliyoandaliwa na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Afrika Mashariki na Pembe za Afrika ni nafasi ya mwisho ya kuokoa makubaliano ya amani nchini humo.
Sison amesema endapo viongozi hao hawatashiriki katika mazungumzo hayo na kuheshimu muda wa mwisho uliowekwa, marekani haitosita kubadilisha msimamo wake wa vipaumbele vya msaada kwa ajili ya makubaliano ya amani na utekelezaji wake.
Mwenyekiti wa kamati inayofuatilia juhudi za kurejesha amani nchini humo ambaye pia ni rais wa zamani wa Botswana, Festus Mogae ameliambia baraza la usalama kwamba anaamini kwa juhudi na ushirikiano wa viongozi wa kanda nchini humo, amani itarejeshwa.
“Naamini kuwa mbinu thabiti za umoja wa Afrika, umoja wa Mataifa, jumuiya za kimataifa na ushirikiano wa viongozi wa Sudan Kusini tunaweza kurejesha msingi uliopotea na kurejesha matumaini ya wananchi”, alisema Mogae.
Sudan Kusini imekuwa na matumaini ya kuwa na amani kufuatia kupata uhuru kutoka kwa taifa la jirani la sudan mwaka 2011, lakini imetumbukia katika machafuko mwaka 2013 Desemba kufuatia vikosi vya rais Salva Kiir kuanzisha mapigano ya kikabila.
Leave a comment