SHIRIKA la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) linatarajia kukusanya kiasi cha Sh.trilioni 1.3 kwa mwaka wa fedha 2018/2019, anaadika Christina Haule.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Profesa Godias Kahyarara amesema hayo wakati akifungua mkutano wa Wakaguzi na Wafanyakazi waliopo kwenye kurugenzi ya uendeshaji kutoka kanda ya mashariki uliofanyika mjini hapa Morogoro.
Kahyarara amesema shirika limeamua kufanya mkutano huo ili kutathmini mambo yatakayofanyika na kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa kufuatia mikoa ya kanda hiyo kuwa na uwezo wa kukusanya asilimia 60 ya mapato yote ya NSSF.
Amesema katika mwaka wa fedha 2016/17, kupitia mikoa hiyo waliweza kukusanya na kufikia kiasi cha makusanyo ya asilimia 64
“Kwa taifa tumeweka malengo ya makusanyo, na tumeweza kukusanya jumla ya Sh. bilioni 60 kwa miezi minane mfululizo kwa mwaka 2016 na kwa mwezi juni pekee tumeweza kukusanya kiasi cha Sh. bilioni 70.2” amesema
Aidha, amesema kwa kutumia fedha hizo wanaweza kuimarisha malipo ya wanachama na pia kuingiza katika ufufuaji wa viwanda hasa kwenye suala zima la kilimo na kumuunga mkono Rais Magufuli.
Amesema tayari wameshatumia kiasi cha Sh. bilioni 8.71 kwa ajili ya kufufua viwanda kikiwemo kiwanda cha kutengeneza chaki Mufindi.
Leave a comment