CHAMA cha ACT-Wazalendo kimeonesha kuridhishwa na marekebisho yaliyofanyika katika sheria za uchaguzi, kikisema masuala sita kati ya 10 yaliyopendekeza katika mchakato huo, yalijumuishwa katika miswada yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akifungua mkutano wa halmashauri kuu ya ACT-Wazalendo, leo tarehe 12 Februari 2024, Kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe amesema hatua hiyo ni muhimu na kwamba wanajipa moyo kuwa mabadiliko hayo ni hatua muhimu katika safari yao ya kudai kuwa na chaguzi huru na zenye haki.
“Mabadiliko ni mchakato sio tukio la siku moja. Siku zote tumeongozwa na maneno ya Mwalimu Nyerere aliyoyatoa Tabora 1958 kwamba “Ni busara ikiwa mtu amedai kiasi fulani kwa mdeni wake, akimlipa sehemu fulani ya kiasi anachodaiwa inafaa kipokewe kiasi hicho na palepale iendelee kudaiwa sehemu iliyobaki. Kwani hata hicho kidogo ni haki yake,”
“ Hivi ndio unaweza kuendelea kulipwa mpaka haki yako yote uipate”. Hivyo basi ni lazima tujipe moyo kuwa mabadiliko haya ni hatua muhimu sana katika safari yetu ya kudai kuwa na chaguzi huru na zenye haki na kuacha alama ya kudumu katika nchi yetu kupitia chama chetu,” amesema Zitto.
Zitto ametaja baadhi ya masuala ambayo yamefanyiwa kazi katika marekebisho hayo, ikiwemo la kuwaondoa wakurugenzi wa jiji, manispaa na halmashauri kuwa wasimamizi wa uchaguzi wa ngazi ya jimbo. Kumwondoa mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi kuwa Katibu wa Kamati ya Usaili pamoja na mwenyekiti na makamu mwenyekiti wa tume ya ucahguzi kutoteuliwa na Rais.
“Baadhi ya mambo hayakukubaliwa na ni jambo la kawaida katika majadiliano yeyote, tungeshangaa kama tungepata yote 10. Mabadiliko ni mchakato sio tukio la siku moja,” amesema Zitto.
Leave a comment