KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameishauri Serikali ianzishe mjadala wa kitaifa kwa ajili ya kujadili namna ya kuandaa dira mpya ya maendeleo kwa miaka 25 ijayo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Zitto ametoa ushauri huo katika mkutano wa maafisa mipango na wachumi wa wizara, idara, mashirika ya umma, mikoa na mamlaka za serikali za mitaa nchi nzima, uliofanyika jijini Arusha, kwa ajili ya kujadili maandalizi ya dira ya taifa ya maendeleo.
“Lazima tuwe na mjadala wa ukweli miongoni mwetu Watanzania bila ubaguzi wa kisiasa kuhusu miaka 25 iliyopita. Je tulikuwa na mwafaka wa kitaifa kuhusu dira? Je, tulikuwa na nidhamu ya kutosha kutekeleza dira ya 2025? Kwanini ilichukua miaka 10 kuanza kutekeleza dira? Tuwe tayari kukubali matobo na kuweka mikakati ya kuziba matobo hayo,” amesema Zitto.
Mwanasiasa huyo amesema kuwa, baada ya mjadala huo kufanyika, mwafaka wa kitaifa ujenge juu ya namna ya kuipeleka Tanzania katika miaka 25 ijayo.
“Lazima na ni muhimu kwa Watu wenye kufanya maamuzi na wenye ushawishi wa kimaamuzi kukubaliana mwafaka wa kitaifa. Hii bargain – ijenge makubaliano ya uhakika kuhusu maendeleo , kujenga dola lenye utayari wa kusaidia maendeleo na sio predatory state, ikubali kujifunza na kurekebisha makosa kila wakati yakitokea,” amesema Zitto.
Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo, amesema kuna haja ya Serikali kuweka mikakati itakayosaidia kukuza uchumi wanchi kwa wastani wa asilimia nane kila mwaka, ili kukidhi ongezeko la idadi ya watu inayokadiriwa kufikia milioni 130 ifikapo 2050
Leave a comment