WATU wenye silaha wamedaiwa kujaribu kumuua Waziri Mkuu wa Haiti, Ariel Henry wakati wa sherehe ya kuadhimisha kumbukumbu ya uhuru wa nchi hiyo siku ya Jumamosi tarehe 1 Januari, 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tukio hilo lilitokea wakati Henry alipokuwa akishiriki katika hafla hiyo katika kanisa moja katika mji wa kaskazini wa Gonaïves.
Video iliyowekwa mtandaoni ilionesha waziri mkuu na msafara wake wakitembea kwa kunyata kuelekea kwenye magari yao huku kukiwa na milio ya risasi.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Associated Press, hali ya usalama imezorota tangu kuuawa kwa Rais Jovenel Moïse Julai mwaka uliopita.
Henry ameahidi kukabiliana na magenge yenye nguvu ambayo yanalaumiwa kwa wimbi la utekaji nyara na kuchukua udhibiti wa sehemu kubwa ya usambazaji wa gesi nchini humo na kusababisha uhaba mkubwa wa mafuta.
Ofisi ya waziri mkuu ilisema majambazi na magaidi ndio waliohusika na jaribio hilo la mauaji, na kwamba vibali vya kukamatwa vimetolewa kwa washukiwa hao.
Ofisi hiyo ilishutumu kundi hilo kwa kujificha nyuma ya kuta kushambulia msafara huo na kutishia askofu kwa kuzingira kanisa.
Mtu mmoja aliuawa na wengine wawili kujeruhiwa katika mapigano ya risasi kati ya watu wenye silaha na vikosi vya usalama, vyombo vya habari vya ndani viliripoti.
Shambulio hilo ni pigo jingine kwa utawala unaoongozwa na Henry, ambaye alikua kaimu mkuu wa serikali ya Haiti wiki mbili baada ya Moïse kuuawa. Mazingira ya jaribio la mauaji hayo yanayoaminika kutekelezwa na kundi la wanamgambo lakini bado hawajafahamika.
Tarehe ya kupiga kura kumchagua rais mpya bado haijatangazwa.
Kuongezeka kwa ghasia na hali mbaya ya kiuchumi, iliyofanywa kuwa mbaya zaidi na majanga kadhaa ya asili katika miaka ya hivi karibuni, imesababisha idadi kubwa ya Wahaiti kutafuta fursa katika nchi nyingine.
Leave a comment