WATU wanne wanashikiliwa na Jeshi la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, kwa tuhuma za mauaji ya Shaban Amiri Mbalali (20), yaliyotokea tarehe 31 Julai 2021, maeneo ya Chamanzi Vigoa mkoani Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatano, tarehe 4 Agosti 2021 na Kamanda wa Jeshi la Polisi la kanda hiyo, ACP Jumanne Muliro, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Kamanda Muliro amewataja watuhumiwa hao kuwa, ni Anold Peter Kavishe (36), mkazi wa Maji Matitu. Jastin Joseph (32), mkazi wa Kisewe. Selemani Hamisi (39), mkazi wa Chamanzi na Joyce John (39) , mkazi wa Maji Matitu.
“Jeshi la Polisi linawashikilia watu wanne kwa tuhuma za kumuua Mbalali, mchunga mbuzi na aliyekuwa mkazi wa Chamazi,” amesema Kamanda Muliro.
Kamanda Muliro amedai kuwa, watuhumiwa hao baada ya kumuuwa Mbalali, mwili wake waliufukia kwenye shimo, kisha wakaiba mbuzi watano aliokuwa anachunga.
“Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, lilianza ufuatiliaji mara moja na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao, wakiwa na vielelezo kadhaa,” amesema Kamanda Muliro.
Kamanda Muliro amesema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani, kujibu tuhuma za mauaji zinazowakabili.
Leave a comment