WATU wenye ulemavu nchini Tanzania, wameiomba Serikali iongeze ushiriki wao katika vyombo vya maamuzi ili waweze kutafuta suluhu dhidi ya changamoto zinazowakabili. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa Leo Jumamosi, tarehe 10 Desemba 2022 na kundi hilo wakizungumza na MwanaHALISI Online kuhusu maadhimisho ya siku ya haki za binadamu duniani.
Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Uwezsshaji (KIOO) mkoani Kigoma, Edward Saimon, amesema kukosekana kwa ushiriki wa walemavu katika vyombo vya maamuzi, kunarudisha nyuma kimaendeleo.
“Kwa kuwa hatushiri kwenye vyombo vya maamuzi kila anayekuja anasema anatusaidia. Hoja inabaki anatusaidiaje wakati sisi sio sehemu ya huo mchakato wa usaidizi? Fikiria CCM kwa mfano kama chama tawala wana wing ya vijana, wanawake na wazazi lakini kwa makusudi hawana wing ya watu wenye ulemavu,” amesema Saimon.
Saimon ameiomba Serikali itoe ruzuku maalum Kwa watu wenye ulemavu ili wajiendeleze kiuchumi “Serikali inatoa ruzuku kwa vyama vya siasa Sina uhakika kwa vyama vya watu wenye ulemavu. Waziri mwenye dhamana ya watu wenye ulemavu ni mtu mzima tafsiri yake ni nini? Mbona waziri wa wanawake sio mwanaume? Shida ya pili hiyo. Ni uthibitisho wa kubaki nyuma.”
“Kwenye serikali za mitaa kuna mikopo kwa watu wenye ulemavu ambayo ni 2% ya mapato ya ndani lakini masharti wa watu wenye ulemavu ni sawa na kwamba serikali wala wadau hawataki walemavu kushiriki.
Wakijua walemavu wana changamoto zisizofanana lakini vigizo kwa karibu kila kitu vinafafanana. Mfano bodi ya mikopo, unampa mlemavu mkopo wa elimu ya juu bila kujali ataajiliwa au la Nini matokeo yake? Hivi kwanini tumkopeshe badala ya kumwezesha na kumdai matokeo?” Amehoji Saimon na kuongeza:
“Sheria ya ajira na mahusiano kazini inataka mwajiri mwenye wafanyakazi zaidi ya 20 kuhakikisha kwamba 3% yao ni watu wenye ulemavu tujiulize ni mwajiri gani aliyekidhi takwa hili la kisheria? Kama yupo ni nani kama hayupo Nini kimefanyika juu yao.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Sauti ya Wanawake Wenye Ulemavu Tanzania (VODIWOTA), Stella Jairos, amesema kundi Hilo linakabiliwa na changamoto nyingi ambazo Serikali inatakiwa izitafutie ufumbuzi wa haraka.
Akitaja baadhi ya changamoto hizo, amesema baadhi ya wanawake walemavu hukabiliwa na ukatili wa kijinsia wanapokwenda kupata huduma za afya hasa ya uzazi ambao huonekana kama hawana haki ya kupata watoto kutokana na ulemavu wao.
“Changamoto ziko nyingi Tena nyingi sana, zile changamoto za ukiukwaji wa haki za binadamu zinazowakabili watu wasiokuwa na ulemavu, kwetu sisi ziko maradufu yake. Mlemavu akienda hospitali kujifungua anapewa kauli za kashfa kama vile Hana haki ya kupata mtoto,” amesema Stella.
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa, amesema changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu zimekithiri Kwa kuwa hakuna nguvu ya kutosha katika kuwatetea.
“Hali ya utetezi wa haki za walemavu Iko chini sana na takwimu za idadi yao haijakaa sawa. Mashirika yanayowatetea Yako chini hayajajengewa uwezo,” amesema Olengurumwa na kuongeza:
“Kama mtandao tumeamua kuanzisha dawati la watu wenye ulemavu Ili kuwasikiliza na kushughulikia matatizo Yao. Pamoja na kuwajengea uwezo Ili waweze kijitetea.”
Kwa mujibu wa kundi Hilo, walemavu bado wanakabiliwa na changamoto za kukosa elimu, ajira, huduma msingi za kijamii, kitendo kinachosababishwa na ukosefu wa miundombinu rafiki ya kutolea huduma.
Kuhusu changamoto ya ukosefu wa elimu, Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, ilielekeza fedha Sh. 960 milioni, zilizopangwa kwa ajili ya sherehe za kitaifa za maadhimisho ya miaka 61 ya uhuru, kwa ajili ya kujenga mabweni katika shule nane za msingi za watu wenye mahitaji maalum.
Leave a comment