SERIKALI ya Tanzania, imesema itafanya uchunguzi dhidi ya biashara haramu ya uuzaji viungo vya siri vya wanawake wanaokeketwa, iliyoibuka mkoani Mara. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa Leo Jumamosi, tarehe 10 Desemba 2022 na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima, baada ya kupokea ripoti ya msafara wa siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia nchini.
“Kuhusu biashara ya watu hili ni jambo kubwa sana, ahsanteni Kwa kuliibua. Mtu atasema tumejuaje? Tunaenda kuchunguza tujue hivi vitu kwamba sio tu mila bali ni biashara kubwa, limegeuka kutoka kwenye Mila kwenda kishirikina,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwajima amesema “nitoe wito kwa waganga wa kienyeji wanaofanya utapeli kwenye jamii kuuza viungo vya watu vya Siri wanavyonyofoa wakati wa ukeketaji. Wanachukua na kufanyia shughuli za biashara. Nitazungumza na waziri wa mambo ya ndani ya nchi Ili kuchunguza tupate ushahidi.”
Ripoti hiyo inadai kuwa, wasichana wanaokeketwa viungo vyao huuzwa kwa wafanyabiashara wakubwa wa madini na wavuvi, Kwa Imani kwamba wakivitumia vinaongeza madini na samaki.
Ripoti hiyo inadai kuwa, viungo hivyo huuzwa kati ya Sh. 1,000,000 Hadi 20,000,000, kutegemeana na wingi wa viungo hivyo.
“Hii ina maana kuwa tatizo la ukatili wa kijinsia ni zaidi ya Mila na desturi kama ilivyozoeleka. Hivyo upo umuhimu wa Serikali na wadau kufanya utafiti Ili kugundua wanaonufaika na biashara hii wachukuliwe hatua za kisheria,” imesema ripoti hiyo.
Aidha, ripoti hiyo imeibua matukio ya ukatili wa kijinsia ikiwemo ubakaji, ulawiti, ndoa za utotoni, ajira za utotoni, rushwa ya ngono, ukeketaji, vipigo, matusi, utekelezwaji wa familia, wanandoa kunyimana tendo la ndoa na walemavu kubaguliwa katika nyanja mbalimbali.
Kufuatia uibukaji wa matukio hayo, Dk. Gwajima ametangaza vita Kwa watu wanaovitekeleza.
“Wote wenye mpango wa kufunga sauti za watetezi wa haki za binadamu na kusababisha machozi ya wanawake na watoto kutiririka bila kufutwa, waache mara Moja. Tutachukua hatua Kwa mujibu wa Sheria na kanuni, siko tayari kumlinda anayekandamiza wanawake na watoto,” amesema Dk. Gwajima.
Aidha, Dk. Gwajima amesema wizara yake inaangalia uwezekano wa kufumua muongozo wa kamati zinazosimamia masuala ya ustawi wa jamii ngazi za chini, Ili kutoa nafasi Kwa Mashirika Yasiyokuwa ya Kiserikali (NGO’s), kushiriki.
Aidha, Dk. Gwajima amesema Rais Samia Suluhu Hassan, amemuagiza kushughulikia vitendo vya ukatili wa kijinsia Kwa kuwa anakerwa navyo.
Kufuatia agizo Hilo, Dk. Gwajima ametangaza siku 365 za kutokomeza vitendo hivyo, kuanzia Leo, huku akisema wizara yake Iko katika hatua za mwisho za kumalizia uandaaji mpango mkazi wa pili wa kutokomeza ukatili wa kijinsia ambapo unatarajiwa kuzinduliwa Februari 2023.
Katika hatua nyingine, Dk. Gwajima amewataka Watanzania bila kujali tofauti zao, kushirikiana katika kutokomeza matukio ya ukatili wa kijinsia kwa kuwa wanaothirika ni watoto wa wanachama wa vyama mbalimbali vya siasa.
Leave a comment