BAADHI ya akina mama wajawazito katika Kituo cha Afya cha Buzuruga, kilichopo Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela Jijini Mwanza, wanadaiwa kujifungulia chini kwenye sakafu kutokana na uhaba wa vitanda. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Taarifa hizo zimesambaa hivi karibuni kwenye mitandao ya kijamii, huku kukiwa na picha zinazoonesha baadhi ya wajawazito wakiwa katika chumba kinachodaiwa kuwa cha kujifungulia huku wengine wakiwa wamelala chini wakisubiri huduma.
Inadaiwa kuwa, picha hiyo imepigwa na mjamzito mmoja aliyeingia na simu kwa siri baada ya uongozi wa kituo hicho kupiga marufuku ya kuingia na simu ili kuzuia watu wasipige picha.
Hata hivyo, leo tarehe 18 Disemba 2023, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Wakili Kiomoni Kibamba, amekanusha uwepo wa tukio hilo akidai hakuna mjamzito anayejifungulia chini kwa kuwa vitanda vimeongezwa kituoni hapo.
Taarifa hiyo imedai, awali kituo hicho kilikuwa na vitanda vitatu kwa ajili ya kujifungulia kitendo kilicholeta changamoto hivyo Serikali iliongeza hadi kufikia sita.
“Hivyo kwa maelezo hayo, Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela inapenda kuuhakikishia umma kuwa katika Kituo cha Afya cha Buzuruga, hakuna wakina mama wanaojifungulia chini kama taarifa ya mtandaoni inavyoeleza,” imesema taarifa ya Wakili Kibamba.
Kuhusu picha iliyosambaa mitandaoni, taarifa ya Wakili Kibamba imesema sio ya hivi karibuni kama inavyodaiwa, bali ilipigwa Septemba 2022.
Kabla ya taarifa hiyo kutolewa, MwanaHALISI Online ilimtafuta Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu kwa njia ya simu ili kupata ufafanuzi wa tukio hilo, lakini simu yake haikupokelewa. Ilipomtafuta Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel simu yake haipatikani hewani.
Tuache kusema uongo mweupe. Baada ya video ndipo ukaongeza vitanda. Mbona takwimu hukutumia kutuambia walikuwa wangapi na ukakubali kulikuwa na ongezeko la wajawazito. Hivi siyo vitu vya kuficha.
Mama hawezi kuongeza hospitali mkiendelea kudanyanya hivi.