KATIKA mwendelezo wa kuadhimisha mwezi wa huduma kwa wateja, wafanyakazi sita wa Benki ya NMB jana wameanza safari ya siku saba ya kupanda Mlima Kilimanjaro kupitia geti la Machame ambapo wataipeperusha bendera ya benki hiyo katika kilele cha mlima huo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza katika hafla ya kuwaaga na kuwakabidhi rasmi bendera wafanyakazi hao, Ofisa Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA), Charles Ng’endo alisema KINAPA wamefarijika na utaratibu uliofanywa na NMB katika kuadhimisha mwezi huu muhimu wa huduma kwa wateja kwa kupanda Mlima Kilimanjaro.
Aidha, aliahidi kuwa uongozi wa hifadhi hiyo utahakikishia kuwa wamewawekea mazingira mazuri na utaratibu mzuri wa kuwahudumia mpaka wanafika kileleni.
Aliongeza kuwa “kufanya hivi kunatusaidia kutangaza utalii wa ndani na tunafahamu hifadhi ya Taifa TANAPA na NMB tumekuwa na uhusiano ya karibu ya kibiashara na utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Hivyo, kupanda Mlima Kilimanjaro na kufika kileleni kutaimarisha uhusiano kati yetu sote na kupeleka ujumbe kwa wateja wetu kuweza kutangaza utalii wa ndani,” alisema.
Naye Meneja wa benki hiyo Kanda ya Kaskazini-Dismas Prosper alisema NMB kwa kutambua umuhimu wa sekta ya Utalii hapa nchini, waliona ni jambo la kifahari kusherehekea mwezi wa huduma kwa wateja pamoja na wateja wao ambao wapo katika safari hiyo kwa kupanda mlima Kilimanjaro ili kuutangaza mlima huo.
Alisema timu hiyo imepandishwa Mlima na kampuni ya Zara tours yenye uzoefu wa miaka mingi.
Aidha, Kiongozi wa msafara huo wa wafanyakazi wa NMB ambaye pia ni Afisa Mkuu wa Wateja Wakubwa wa NMB – Alfred Shao alisema NMB imefanya mambo mengi makubwa hapa nchini ikiwamo kuwa Benki bora na yenye masuluhisho mengi ya kifedha kwa wateja wao.
Pia aliongeza kuwa, safari hiyo ya kupanda mlima Kilimanjaro inamaanisha kwamba, NMB wanaudhihirishia umma na wateja wao kuwa wanao uwezo wa kuwahudumia mpaka kilele cha Mlima Kilimanjaro na wajue wanamaanisha wanaposema ‘NMB Karibu Yako’.
Wengine waliopanda Mlima ni Nishad Jinah, Stella Motto, Reginald Baynit, Agnes Mlolele na Christopher Mwalugenge.
Leave a comment