WABUNGE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), leo tarehe 10 Septemba, 2022 wanatarajiwa kufanya uchaguzi wa ndani wa wagombea wa ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), kabla ya kwenda kupigiwa kura bungeni na wabunge wote tarehe 13 Septemba, mwaka huu. Anaripoti Erick Mbawala, TUDARCo … (endelea).
Taarifa iliyotolewa iliyotolewa jana tarehe 9 Septemba, 2022 na Katibu wa NEC – Itikadi na uenezi CMM, Shaka Hamdu Shaka imeeleza kuwa hatua hiyo imefikiwa baada ya wagombea kupendekezwa na Kamati Kuu ya CCM (CC).
Shaka amesema wagombea wote wanapaswa kuwepo makao makuu ya CCM Dodoma leo.
“Kwa mujibu wa kanuni za CCM za uteuzi wa wagombea wa CCM katika vyombo vya dola, uteuzi wa wagombea nafasi za ubunge wa Afrika Mashariki utafanywa na kamati ya wabunge wote wa CCM,” amesema Shaka.
Shaka amesema jumla ya wanachama 16 wameteuliwa na kupendekezwa kuwania nafasi tano za ubunge wa EALA ambapo kati ya nafasi hizo watatu ni wanaume na wawili wanawake.
Amewataja wanaume walioteuliwa na kupendekezwa na Kamati Kuu kuwa ni pamoja na Dk. Gilbert Bankobeza, Anar Kachwamba, Benedict Kivove, Dk. Ng’waru Maghembe, Gidion Mandesi, Methusela Mbajo, Brigedia Jenerali Marianus Mhagama, Balozi James Msekela, Dk Leonard Subi na James Millya.
Kwa upande wa wanawake, walioteuliwa kuwania nafasi mbili ni Theddy Patrick, Angela Kizigha, Dk Shogo Mlozi, Doris Mollel, Amina Mgeni na Jalia Mayanja.
Aidha, kwa upande wa Zanzibar, wabunge hao wa CCM watateua na kupendekeza wanachama watatu ambapo wawili watakuwa wanaume na mmoja mwanamke.
Wanaume walioteuliwa kuwania nafasi hizo tatu ni Machano Ali Machono, Abdulla Hasnuu Makame, Mmanga Miengo Mjawiri, Mourice Oscar Bendera, Haji Vuai Ussi, Faki Ame Kesi.
Wanawake kutoka Zanzibar waliopitishwa na CC ni Lulua Salum Ali, Nadra Juma Mohamed, Maryam Said Mussa na Rahma Mohamed Ibrahim.
Leave a comment