AJALI ya gari iliyotokea usiku wa kuamkia tarehe leo 26 Machi 2024, maeneo ya Nyamwage mkoani Pwani, imekatisha maisha ya waandishi wa habari wawili, waliokuwa wanatokea Dar es Salaam, kuelekea mkoani Lindi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Waandishi waliofikwa na umauti katika ajali hiyo ni Abdallah Nanda, mwandishi wa habari wa kituo cha runinga cha Chanel Ten na Josephine Kibiriti, aliyekuwa mwandishi wa Kampuni ya Sahara Media Group inayomiliki vituo vya habari mbalimbali ikiwemo Star Tv.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Rufiji, SACP Protas Mutayoba, chanzo cha ajali hiyo ni gari walilokuwa wanasafiria waandishi hao kugongana na lori la mizigo, huku uzembe ukitajwa kuwa sababu kuu.
“Miili ya marehemu imehifadhiwa katika Kituo cha Afya cha Ikwiriri pamoja na majeruhi mmoja anaendelea kupatiwa matibabu kituoni hapo,” amesema Kamanda Mutayoba.
Mbunge wa Mtama, Mkoa wa Lindi, Nape Nnauye, amesema vifo vya wanahabari hao ambao enzi za uhai wao walikuwa wanafanya kazi mkoani humo, vimeacha pigo.
“Ajali imesababisha pigo kubwa kwa sekta ya habari na kwa wana Lindi usiku wa kuamkia leo. Ndio kwanza kama ni mti ulianza kutoa maua tayari kwa matunda, ghafla mmezimika kama mshumaa, pumzikeni kwa amani,” ameandika Nape katika ukurasa wake wa mtandao wa X.
Leave a comment