SERIKALI ya Urusi imefungua milango ya ushirikiano wa kiuchumi, kijamii na teknolojia, kwa mataifa ya Afrika, huku ikiahidi kutoingilia masuala yake ya ndani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamebainishwa jana tarehe 29 Septemba 2023, jijini Dar es Salaam na Balozi wa Urusi nchini Tanzania, Andrey Avetisyan akitangaza matokeo ya matokeo ya mkutano wa pili wa mataifa ya Afrika na Urusi, uliofanyika mwishoni kwa Julai 2023 nchini humo.
Balozi Avetisyan alisema katika mkutano huo uliohusisha maelfu ya viongozi wakiwemo 2,000 kutoka nchi rafiki 27 za Afrika, masuala mbalimbali yalijadiliwa kabla ya kuwekewa maazimio au mikataba yake kusainiwa.
Alitaja masuala hayo kuwa ni, uchumi mpya wa dunia, ushirikiano katika sayansi na teknolojia, misaada ya kibinadamu na kijamii, ulinzi na usalama, pamoja na namna ya kuboresha maisha ya wananchi.
Balozi Avetisyan alisema katika mkutano huo uliokuwa na sehemu mbili, wakati wa mjadala wazungumzaji walieleza dhamira yao ya kufanya kazi pamoja katika kujenga uhudiano mzuri wenye haki baina ya pande zote mbili, hususan uhuru wa Mamlaka za nchi washirika.
“Huu ni ujumbe muhimu kwa dunia ya leo, kwa bahati mbaya hatutaweza kusikia popote katika nyakati hizi,” alisema Balozi Avetisyan.
Alisema matunda ya mkutano huo ni maazimio manne yaliyowekwa na washiriki, uzinduzi wa jukwaa la Urusi-Afrika kwa 2023-2026.
Matunda mengine ni utiaji Saini nyaraka mbili muhimu, ushirikiano wa Kiserikali kwenye maendeleo (IGAD) na Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika ya Kati (ECCAS).
“Katika mkutano huo Rais Putin aliahidi kushirikiana na viongozi wa Afrika kuleta maendeleo ya pande zote mbili,” alisema Balozi Avetisyan.
Leave a comment