MASHIRIKA Yasiyo ya Kiserikali (NGO’S), yanayotetea haki za binadamu, yamelaani uamuzi wa Kamati ya Maadili ya Mawakili, kumsimamisha uwakili, Mpale Mpoke, kwa muda wa miezi sita, ikidai unalenga kuminya tasnia ya sheria. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Miongoni mwa mashirika hayo ni Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).
Mpoki alisimamishwa uwakili jana tarehe 20 Novemba 2023 na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Mawakili, Jaji Ntemi Kilikamajenga, wakati anaongoza jopo la mawakili wa utetezi, katika shauri linalomkabili Wakili Boniface Mwabukusi, mbele ya kamati hiyo iliyoketi kwenye Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa tamko la mashirika hayo, Mpoki alipewa adhabu hiyo baada ya kutangaza nia ya mteja wake kukata rufaa dhidi ya uamuzi mdogo uliotolewa na kamati hiyo juu ya mapingamizi ya awali yaliyowekwa na Wakili Mwabukusi kupinga maombi ya AG yaliyotaka avuliwe uwakili.
“Tunasisitiza kuwa, kusimamishwa kwa leseni ya uwakili ya Mpoki ni ukiukwaji wa haki zake kama wakili. Ukiukwaji wa kanuni ya haki ya usawa wakati wa usikilizwaji wa shauri. Kumsiamisha kazi wakili kwa kueleza nia ya mteja wake kukata rufaa kunadhoofisha uadilifu wa taaluma ya sheria,” imesema tamko la NGO’s hizo.
Mashirika hayo yameitaka kamati hiyo kufikiria upya uamuzi wake wa kumsimamisha uwakili Mpoki, ikiwa pamoja na kutengua adhabu hiyo kwa madai kuwa inakwenda kinyume na kanuni za haki.
Mwanasheria hiyo maarufu nchini, alikuwa anamtetea Wakili Mwabukusi, katika shauri alilofunguliwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) mbele ya kamati hiyo, ikimtuhumu kutoa lugha za kushambulia viongozi wakati anazungumzia mkataba wa uwekezaji bandarini.
Mpoki ni wakili mwandamizi nchini, aliyedumu katika majukumu yake kwa zaidi ya miaka 34, tangu aliposajiliwa Desemba 1989, ambapo ameshawahi kuwa makamu wa rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS), kati ya 2011 hadi 2012 na 2019 hadi 2021.
Leave a comment