CHAMA cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), kimetangaza kuondoa uwakilishi wake kwa muda katika Kamati ya Maadili ya Mawakili, hadi pale hatma ya Mpale Mpoki, aliyesimamishwa uwakili kwa kipindi cha miezi sita, itakapojulikana. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Uamuzi huo umetangazwa leo tarehe 21 Novemba 2023 na Rais wa TLS, Harold Sungusia ikiwa ni siku moja tangu Mpoki apewe adhabu hiyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Mawakili, Jaji Ntemi Kilikamajenga.
“Kwa mujibu wa mamlaka ambayo Baraza la Uongozi limepewa chini ya kifungu namba 16(a)(j), cha Sheria ya Chama cha Sheria Tanganyika, sura na. 307 kikisomwa kwa pamoja na kifungu cha 4(1) (c) cha Sheria ya Mawakili sura na. 341 na limefanya uamuzi wa kuondoa kwa muda uwakilishi wake katika Kamati ya Maadili ya Mawakili, mpaka pale itakapoamuliwa vinginevyo,” imesema taarifa ya Sungusia.
Mbali na uamuzi huo, taarifa ya Sungusia imesema, Baraza la Uongozi la TLS, limemteua mjumbe wake, Stevephen Mwakibolwa, kujiunga katika jopo la mawakili wanaomuwakilisha Wakili Mpoki katika rufaa yake ya kupinga kusimamishwa uwakili kwa muda.
Pia, taarifa ya Sungusia imesema, TLS itateua mawakili wengine kwa ajili ya kumwakilisha Wakili Mwabukusi, katika shtaka analokabiliwa la kutoa lugha za kushambulia viongozi wa serikali wakati anajadili sakata la mkataba wa uwekezaji bandarini.

Kwa mujibu wa TLS, Jaji Kilikamajenga alitoa uamuzi wa kusmiamisha uwakili Mpoki, jana Jumatatu wakati mwanasheria huyo mwandamizi anamtetea Wakili Boniface Mwabukusi, katika shauri alilofunguliwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
TLS inadai kuwa, Mpoki alisimamishwa uwakili kwa kosa la kukiuka maadili ya uwakili, baada ya kuijulisha kamati hiyo kuhusu nia ya kukata rufaa kutokana na mapingamizi ya awali waliyoweka dhidi ya AG ili kumtetea Mwabukusi, kukataliwa.
Leave a comment