SERIKALI ya Tanzania, imezitaka pande mbili zinazosigana nchini Sudan na kusababisha mapigano yaliyogharimu maisha ya watu zaidi ya 180 na majeruhi 1,000, ziketi mezani kwa ajili ya kutafuta muafaka kwa njia ya amani na usalama. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 19 Aprili 2023, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Stergomena Tax, akitoa msimamo wa Tanzania kuhusu mapigano hayo yaliyoibuka tarehe 15 Aprili mwaka huu, kati ya vikosi vya Serikali na vikosi vya misaada.
Dk. Tax amesema, Tanzania inaunga mkono tamko lililotolewa na Baraza la Amani la Usalama la Umoja wa Afrika (AU), lilitolewa tarehe 16 Aprili 2023, kulaani mapigano hayo ambayo yalisitishwa kwa saa 24 kuanzia jana jioni.
“Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaunga mkono tamko lililotolewa na Baraza la Amani la Usalama la Umoja wa Mataifa kulaani mapigano yanayoendelea Tanzania, inazitaka pande zote mbili zinazohasimiana kutatua mgogoro huo kwa njia ya amani na usalama, huku ikihakikisha haki na usalama wa raia,” amesema Dk. Tax.
Waziri huyo wa mambo ya nje, amesema hakuna mtanzania aliyepoteza maisha au kujeruhiwa, huku akisema Serikali inafuatilia ili kuandaa mpango wa kuwaondoa raia wa Tanzania nchini humo kama hali haitakuwa shwari.
“Tunao Watanzania takribani 210, hadi sasa hakuna Mtanzania aliyeripotiwa kujeruhiwa na mapigano hayo. Serikali inachukua hatua kuhakikisha watanzania wanakuwa salama na tunaendelea na juhudi hii. Hadi sasa mapigano yamesitishwa kwa saa 24 kuanzia jana jioni kutoa fursa za mahitaji ya kibinadamu,” amesema Dk. Tax na kuongeza:
“Kufuatia juhudi zinazoendelea uko uwezekano na muelekezo uliopo ni kusitisha mapigano kutatua mgogoro kwa amani, Serikali inafuatilia kuandaa mpango wa kuwachukua raia wa Tanzania kadri itakavyohitajika.”
Leave a comment