SERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha uhusiano wenye manufaa kwa pande zote mbili ili kuendelea kufungua milango ya fursa za kibiashara zitokanazo na diplomasia ya uchumi. Anaripoti Gabriel Mushi, Ankara- Uturuki…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 18 Aprili 2024 na Rais Samia Suluhu Hassan katika mkutano na waandishi wa habari pamoja na rais mwenyeji wake wa Uturuki, Recep Tayyip Erdoğan, katika Ikulu ya Ankara nchini Uturuki.
Aidha, katika hafla hiyo, wakuu hao wawili wa nchi walishuhudia utiaji saini wa Hati sita za Makubaliano (MoU) ambazo zitarahisisha ushirikiano katika maeneo ya elimu ya juu, ushirikiano wa kiuchumi na kubadilishana utamaduni.
Ili kutekeleza mikataba hiyo iliyoafikiwa, Rais Samia alibainisha kuwa wamewaelekeza mawaziri wenye dhamana na timu zao za wataalamu kukutana na kuja na mkakati wa kuweka mikakati ya utekelezaji wa maeneo ya ushirikiano.
“Türkiye imekuwa mshirika wa thamani na Tanzania; hivyo basi, ziara yangu mjini Ankara inasisitiza kujitolea kwangu kuthamini ushirikiano huu,” alisema.
Kuhusu uhusiano uliopo baina ya nchi hizo, aliongeza kuwa umefungua njia kwa wataalamu wa Uturuki kuchangia katika kuleta mabadiliko ya Tanzania kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ikiwemo ya reli ya kisasa (SGR) inayounganisha Tanzania na nchi nyingine jirani.
“Kuhusu kukuza biashara na uwekezaji, Tanzania inalenga kushirikiana na sekta binafsi ya Uturuki, na tutakutana kesho Istanbul.
“Ushirikiano utazingatia jumbe tatu muhimu: kuwafahamisha juu ya athari chanya ambayo wawekezaji na wafanyabiashara wa Uturuki wanaleta katika nchi yetu, kuwaeleza mazingira ya biashara nchini Tanzania, na kuelezea nafasi ambayo Tanzania inaweza kutoa kukuza biashara. Tunawakaribisha wawekezaji wa Uturuki, hasa katika nyanja za viwanda, kilimo, na utalii,” Rais Samia alisema.
Katika mkutano wa tete-a-tete na Rais wa Türkiye, Rais Samia alijadili masuala muhimu ya kimataifa, ikiwa ni pamoja na mzozo wa Palestina.
“Tunasisitiza wito wetu wa kusitishwa mara moja kwa vita nchini Palestina,” alisema.
Kwa upande wake, Rais wa Uturuki alisema kuwa uhusiano uliopo hauonyeshi kiwango cha biashara kati ya nchi hizo mbili, na hivyo mipango ya sasa inalenga kuongeza kiwango cha biashara kati ya nchi hizo kufikia dola bilioni 1 za Kimarekani.
Ameongeza kuwa uhusiano wa dhati ulioanzishwa kati ya pande hizo mbili unaimarisha azma yao ya kupambana na changamoto mbalimbali duniani.
Rais Samia yupo nchini Uturuki kwa ziara ya kitaifa ya siku tano kuanzia tarehe 17 hadi 21 Aprili mwaka huu.
Leave a comment