SERIKALI ya Tanzania na Poland, zimekubaliana kupanua wigo wa ushirikiano katika masuala ya biashara na uwekezaji, katika sekta za kimkakati. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 9 Februari 2024 na Rais Samia Suluhu Hassan, akitoa mrejesho wa mazungumzo kati yake na Rais wa Poland, Andrzej Duda aliyeko nchini kwa ziara ya kikazi.
“Kuhusu ushirikiano tulikuwa na mazungumzo mazuri kuhusu maeneo ya kushirikiana kwenye nyanja za elimu, kilimo, biashara na uwekezaji na utalii lakini pia kwenye maeneo ya TEHAMA sababu wenzetu ni wazuri kwenye eneo hilo.
“Tumekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo na kuhamasisha uwekezaji zaidi kwenye sekta za kimkakati kama vile viwanda vya uzalishaji nishati, madini, gesi asilia na uchumi wa buluu,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema Poland imekuwa mshirika mzuri wa maendeleo wa Tanzania ambapo imekuwa ikisaidia katika sekta ya afya kwa kutoa fedha za miradi kwenye hospitali tano za Dar es Slaam. Pia amesema nchi hiyo kutoa bima za benki za biashara kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kwa vipande vya Makutupora, Tabora hadi Isaka.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amewaita wawekezaji wa Poland kuja kuwekeza nchini kwa kuwa kuna fursa nyingi za uwekezaji hususan katika sekta ya utalii kwa kuwa raia wa taifa hilo wanaongoza kwa kuja kutalii Tanzania.
Naye Rais Duda amesema “katika hii miaka ya karibu na kwa safari hii ya kuja Dar es Salaam, nimeweza kuongea na rais kuhusiana na mahusiano yetu kiuchumi na namna gani tunaweza kuyajenga na kutanua mipaka ya mahusiano haya kufikia maeneo mengine yatakayotuletea faida hasa tukifanya kazi na wafanyabiashara.”
Leave a comment