Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dk. Selemani Jafo amesema tangu kuanzishwa kwa Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) mwaka 2006, hoja 25 zimejadiliwa na kati ya hizo 22 tayari zimepatiwa na kuondolewa kwenye hoja za muungano. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Dk. Jafo ametoa kauli hiyo leo Ijumaa bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Najma Murtaza Giga (CCM) aliyetaka kujua mikakati ya Serikali ya kuhakikisha changamoto za Muungano ambazo hazijapatiwa ufumbuzi hazileti madhara nchini na lini zitapatiwa ufumbuzi.
Akiendelea kujibu swali hilo, Dk. Jafo amesema SJMT na SMZ zimetengeneza utaratibu wa kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali za Muungano kupitia vikao vyake.
Amesema kuwa Serikali hizo mbili ziliunda Kamati ya Pamoja ya kutatua changamoto za Muungano ambayo huundwa na wajumbe kutoka pande zote mbili za Muungano.
Aidha, ameongeza kuwa hoja mbili zilizobaki katika orodha hiyo zipo katika hatua za kupatiwa ufumbuzi kupitia kamati hiyo inayoundwa na wajumbe kutoka SJMT na SMZ.
Aidha, Dk. Jafo amesisitiza kuwa Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan na Serikali inayoongozwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi wana nia ya dhati ya kuzitafutia ufumbuzi hoja hizo mbili zilizobaki.
Kwa upande Giga ametoa pongezi kwa Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutatua changamoto za Muungano na kuonesha imani kuwa zilizobaki zitatafutiwa.
Leave a comment