RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu hassan, amesema atalifanyia kazi ombi la Taasisi ya Moyo ya jakaya Kikwete (JKCI), la kuajiri watalaam 12 wa magonjwa ya moyo, kutoka nje ya nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia amesema hayo leo Jumamosi, tarehe 12 Juni 2021, akizindua mitambo miwili ya kisasa ya uchunguzi na tiba ya moyo ya JKCI, iliyosimikwa kwa Sh.4.6 bilioni.
“Kuhusu ombi la kibali cha ajira za wataalamu 12 kutoka nje, ikiwemo wanaofanya kazi za madaktari bingwa watatu, tumepokea maombi yote tutayafanyia kazi,” amesema Rais Samia.
Ombi hilo lilitolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Prof. Mohammed Janabi, akielezea changamoto za utendaji wa taasisi hiyo, ikiwemo uhaba wa watalaamu.
Pia, Prof. Janabi alimuomba Rais Samia atoe Sh.2 bilioni, kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa jengo jipya la taasisi hiyo, unaogharimu Sh.4 bilioni.
Kuhusu ombi la fedha hizo, Rais Samia amesema Serikali yake itatoa fedha hizo.
“Mkurugenzi amewasilisha ombi la fedha za ujenzi wa jengo jipya la taasisi linalogharimu Sh.4 bilioni, nataka nimhakikishie kwamba Sh.2 bilioni za Serikali zitapatikana,” amesema Rais Samia.
Leave a comment