TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), nchini Tanzania, imefanikiwa kuokoa Sh. 250.7 bilioni, kwa kuwafanyia upasuaji kwa njia ya tundu ndogo, wagonjwa 7,175, katika kipindi cha miaka mitano (2015-2020). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 12 Juni 2021 na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Prof. Mohamed Janabi, akielezea mafanikio ya taasisi hiyo kwa Rais Samia Suluhu Hassan, katika uzinduzi wa mitambo mipya ya moyo ya taasisi hiyo.
Prof. Janabi amesema, fedha hizo imeokolewa baada ya wagonjwa hao kupatiwa matibabu nchini, badala ya kusafirishwa nje ya nchi.
“Kila mgonjwa tulikuwa tunalipa Dola za Marekani 1,5000 kwa mmoja, ukizidisha kwa kiwango cha kipindi kile tungekuwa tunalipa hela nyingi. Lakini tumefanikiwa kuokoa fedha za kigeni kwa kufanya upasuaji 7, 175 sawa na dola 107,625,000 (Sh. 250.7 bilioni),” amesema Prof. Janabi.
Mtendaji huyo wa JKCI, amesema taasisi hiyo imefanya upasuaji mkubwa wa moyo kwa wagonjwa 2,000, ambao kama wangesafirishwa nje ya nchi, ingechukua miaka zaidi ya 10, kutokana na uwezo wa Serikali kulipia gharama za kuwasafirisha.
“Kipindi cha miaka mitano wagonjwa karibu 2,000 wamefanyiwa upasuaji mkubwa, ingetuchukua miaka zaidi ya mitano, kama tungewasafirisha nje ya nchi na si miaka mitano pekee bali miaka kumi sababu tulikuwa tunasafirisha wagonjwa wa moyo 200, kwa mwaka kwa sababu ya uwezo,” amesema Prof. Janabi.
Akielezea utendaji wa taasisi hiyo, Prof. Janabi amesema, idadi ya wagonjwa wa kliniki wanaopatiwa huduma JKCI imeongezeka kutoka 23,000 mwaka 2015, hadi kufikia 100,000 mwaka 2020. Huku wa kulazwa ikiongezeka kutoka 2,400 (2015) hadi 3,000 (2020.)
Prof. Janabi amesema, kati ya wagonjwa hao, 13 ndiyo wamepoteza maisha.
Leave a comment